2013-11-13 11:12:12

Mkutano wa mabadiliko ya tabianchi unaendelea mjini Varsavia, Poland


Mkutano wa kumi na tisa kuhusu mabadiliko ya tabianchi utakaodumu kwa siku kumi unaendelea mjini Varsavia, nchini Poland, kwa kuwajumuisha wajumbe kutoka katika nchi 195 duniani. Mkutano huu umefunguliwa rasmi hapo tarehe 12 Novemba 2013 na Bwana Abdullah Bin Hamad Al Attiyah, Waziri mkuu wa zamani wa Qatar. Katika hotuba yake ya ufunguzi amezipongeza nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa kwa kuridhia itifaki ya Kyoto.

Wajumbe wanasema, matatizo na changamoto za mabadiliko ya tabianchi ni mwaliko kwa Jumuiya ya Kimataifa kushikamana kwa pamoja ili kutafuta suluhu ya kudumu, kwani majanga yanayoendelea kujitokeza sehemu mbali mbali yanaonesha umuhimu wa kushirikiana kwa dhati, ili kuacha urithi wa kudumu kwa kizazi kijacho.

Mkutano huu unapania pamoja na mambo mengine kuanzisha mchakato wa itifaki ya kimataifa pamoja na udhibiti wa uzalishaji wa hewa ya ukaa, katika mkutano kama huu utakayofanyika mjini Lima kunako mwaka 2014 na hatimaye, kutiwa sahihi na nchi wanachama mwaka 2016 mjini Paris, Ufaransa. Lengo la Umoja wa Mataifa ni kupunguza nguzi joto kwa kiasi cha nyuzi joto mbili, jambo ambalo bado linaonekana kuwa ni tete!







All the contents on this site are copyrighted ©.