2013-11-13 11:45:01

Mchakato wa amani Syria ni cheche za matumaini!


Askofu mkuu Dominique Mamberti, Katibu mkuu wa mambo ya nchi za nje na ushirikiano wa kimataifa mjini Vatican anasema, cheche za kukubali kushiriki katika mchakato wa kutafuta amani nchini Syria kwa njia za kidiplomasia ni jambo linalotia moyo, hasa kwa kuzingatia kwamba, machafuko ya kisiasa na vita yameendelea kusababisha maafa makubwa kwa watu wasiokuwa na hatia.

Majadiliano ndiyo njia pekee inayoweza kusaidia upatikanaji wa amani ya kuduni nchini Syria. Watu wanaendelea kupoteza maisha na mali kutokana na vita. Umoja wa wapinzani wa Serikali kitaifa umeridhia uamuzi wa kushiriki katika majadiliano ya kidiplomasia kimataifa, ili kutafuta suluhu ya kudumu ya vita inayoendelea nchini Syria. Ujumbe wa Vatican una unga mkono juhudi hizi pamoja na kuendelea kutoa misaada ya kibinadamu kwa waathirika wa vita.

Baba Mtakatifu Francisko anafuatilia kwa ukaribu zaidi mateso na mahangaiko ya wananchi wa Syria na Mashariki ya Kati kwa ujumla wake, ndiyo maana tarehe 5 Septemba 2013 aliitisha siku maalum kwa ajili ya kusali na kufunga ili kuombea amani nchini Syria. Wanasiasa wakionesha utashi wa kweli, vita nchini Syria vinaweza kusitishwa na watu wakaanza maisha ya kawaida anasema Askofu mkuu Mamberti.

Jambo la pili ni kusitisha biashara ya silaha nchini Syria kwani biashara hii pia ni kichocheo kikubwa cha machafuko ya kisiasa na kijamii na matokeo yake ni vita na maafa kwa watu wasiokuwa na hatia. Wananchi wa Syria hawana budi kuanzisha mchakato wa upatanisho, haki na amani; kwa kukazia umoja na mshikamano wa kitaifa bila ubaguzi na upendeleo kwa misingi ya kidini.







All the contents on this site are copyrighted ©.