Maboresho ya huduma kwa mama na mtoto Barani Afrika!
Chama cha Madaktari Wamissionari kwa ajili ya Afrika, CUAMM, kinasema, katika mikakati
yake kwa miaka mitano ijayo, kinapenda kuongeza na kuboresha huduma kwa mama na mtoto
katika nchi zile ambazo wanatoa huduma Barani Afrika. Huduma hii kwa sasa inatolewa
kwa wananchi 1,300,000, wengi wao ni wale wanaoishi vijijini nchini Angola, Ethiopia,
Uganda na Tosamaganga, Iringa, Tanzania.
Madaktari wa CUAMM, wanasema, wanapenda
kutoa kipaumbele cha kwanza kwa mama na mtoto kutokana na mchango wao kwa maendeleo
na ustawi wa familia katika ujumla wake. Mikakati hii inakwenda sanjari na utekelezaji
wa Malengo ya Maendeleo ya Millenia ifikapo mwaka 2015, kwa kupunguza vifo vya wanawake
na watoto wenye umri chini ya miaka mitano. CUAMM inashirikiana na wadau mbali mbali
kitaifa na kimataifa katika kufanikisha lengo hili, ingawa bado kuna mengi ya kufanya.