2013-11-12 07:43:49

Lindeni watoto dhidi ya nyanyaso na dhuluma!


Mtaalam wa haki msingi za binadamu kutoka Umoja wa Mataifa Najat Maala M'jid, hivi karibuni ameitaka Serikali ya Benin kuhakikisha kwamba, inasimama kidete kulinda na kutetea haki msingi za watoto ambazo zinapaswa pia kuwa ni sehemu ya ajenda zake za kisiasa.

Kuna maelfu ya watoto wanaonyanyaswa na kudhulumiwa na wahusika wa vitendo hivi vya aibu bado hawajakamatwa ili wafikishwe kwenye mkondo wa sheria. Watoto wamekuwa wakikamatwa na kutumbukizwa kwenye biashara haramu ya binadamu; wanafanyishwa kazi ngumu zinazowadumaza: kimwili na kisaikolojia; watoto hao pia wamekuwa ni vivutio vikubwa vya biashara ya ngono inayoendelea kushamiri nchini Benin, kinyume cha haki msingi za binadamu, utu na maadili mema.

Taarifa hii ni matokeo ya safari ya kikazi iliyofanywa na Bibi Najat Maala M'jid nchini Benin hivi karibuni kwa kukutana na kuzungumza na viongozi wa Serikali, vyama vya kiraia na waathirika wa vitendo hivi vya kinyama. Wasichana nchini Benin ndio waathirika wakuu wa nyanyaso za kijinsia, ingawa kuna sheria zinazodhibiti vitendo vya uhalifu dhidi ya wanawake na watoto, lakini hazitekelezwi na kwamba, kilio na mahangaiko ya watoto nchini Benin hayasikilizwi.

Bibi Najat Maala M'jid anasema, kuna haja ya kuwa na sera makini zinazolinda maisha, ustawi na maendeleo ya watoto nchini Benin, dhidi ya watu wachache wanaotaka kujinufaisha wenyewe kwa njia za nyanyaso na madhulumu. Ili kufanikisha lengo hili kuna haja kwa Serikali na Jumuiya ya Kimataifa kutenga rasilimali fedha na watu ili kurahisisha utekelezaji wa mikakati inayopania kulinda watoto dhidi ya nyanyaso na dhuluma.







All the contents on this site are copyrighted ©.