2013-11-11 11:47:48

Maaskofu wanaangalia vyombo vya mawasiliano ya jamii vinavyoweza kutumika katika Uinjilishaji wa watu barani Ulaya


Uinjilishaji wa roho za watu Barani Ulaya ni mada ambayo imeongoza mkutano wa siku tatu wa Maaskofu wenye dhamana na vyombo vya mawasiliano ya jamii kutoka Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Ulaya, (CCEE). Maaskofu wameangalia kwa kina na mapana changamoto na vyombo vilivyopo vinavyoweza kutumika kwa ajili ya kutangaza Habari Njema ya Wokovu kwa Makanisa Barani Ulaya, eneo ambalo linaendelea kupokea idadi kubwa ya watu kutoka sehemu mbali mbali za dunia.

Mkutano wa Maaskofu umeandaliwa na kudhaminiwa na Tume ya Mawasiliano ya Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Ulaya. Viongozi wakuu wa Kanisa wamepata nafasi ya kuchangia mawazo yao kuhusu changamoto na nyenzo ambazo zinaweza kutumiwa na Mama Kanisa katika dhamana ya utangazaji wa Habari Njema ya Wokovu kwa Mataifa Barani Ulaya.

Askofu mkuu Claudio Maria Celli, Rais wa Baraza la Kipapa la Mawasiliano ya Jamii alipewa wajibu wa kupitia kwa ufupi yaliyojiri katika Hati juu ya Mawasiliano iliyotolewa na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican na maendeleo yake katika kipindi cha miaka 50 iliyopita. Amegusia, historia, mabadiliko na changamoto ambazo zimejitokeza tangu wakati huo. Wajumbe pia wameangalia namna ambavyo Kanisa linaweza kujitosa kunadi Injili katika soko la kimataifa.

Kardinali Martines Sistach anasema, Maaskofu wameangalia kwa pamoja dhamana ya kimissionari mintarafu tamaduni za Ulaya sanjari na maendeleo ya sayansi na teknolojia ya habari kama nyenzo muhimu ya Uinjilishaji. Mitandao ya kijamii ni jukwaa jipya linaloweza kutumiwa kikamilifu na Mama Kanisa katika mchakato wa Uinjilishaji Mpya.

Lakini ni vyombo vinavyohitaji kuwa na mwelekeo mpana zaidi, kwani ni mitandao inayogusa maeneo maalum ya maisha ya watu. Kanisa lisipokuwa makini, linaweza kujikuta kwamba, linatenga idadi kubwa ya watu wasiokuwa kwenye mitandao. Kuna haja bado kwa Mama Kanisa kuhimiza anasema Kardinali Sistach umuhimu wa kufahamiana na kujenga mahusiano ya dhati ndani ya Jamii husika. Jumuiya zinazoundwa kwenye mitandao ziendelee kuwepo, lakini pia wale wasioguswa na mitandao ya kijamii, wasaidiwe kikamilifu kuona utamu wa Injili.

Ili Kanisa liweze kutekeleza barabara dhamana ya Uinjilishaji kwa njia ya mitandao ya kijamii, kuna haja ya kuwaandaa wataalam watakaotekeleza dhamana hii nyeti; kwa kutenga: rasilimali, muda na nguvu zao, ili kuwawezesha watu hao kujisikia kuwa kweli ni sehemu ya Jumuiya ya Kanisa, inayojitahidi kumwilisha Ujumbe wa Injili katika uhalisia wa maisha yao!

Mitandao ya kijamii kama vile twitter na facebook ni muhimu sana kwa watu wazima na vijana wanaoitumia, kwani ni fursa mpya za kuweza kukutana na hatimaye, kujenga uhusiano mbali na mahusiano ya kimapokeo kama yanvyofahamika kwa wengi. Vijana ni watumiaji wakubwa wa mitandao ya kijamii, wanaojenga urafiki na mahusiano na watu wengi kwa wakati mmoja. Kanisa limetambua umuhimu na mchango wa mitandao ya kijamii ndiyo maana linataka kuwekeza zaidi ili kusaidia mchakato wa Uinjilishaji Mpya.

Hapa Kanisa linaangalia vyombo mbali mbali vya mawasiliano ya kijamii vinavyoweza kutumiwa na Kanisa katika mchakato wa Uinjilishaji mpya. wajumbe wa mkutano huu wa siku tatu wamepata pia nafasi ya kutembelea Kanisa kuu la Familia takatifu, wakiongozwa na mhandisi Jordi Bonet aliyeonesha mwingiliano kati ya Liturujia na na kazi za Uhandisi.







All the contents on this site are copyrighted ©.