Uinjilishaji na tunu msingi za maisha ya kifamilia ni kati ya vipaumbele vya Maaskofu
Katoliki Vietnam
Baraza la Maaskofu Katoliki Vietnam katika mkutano wake wa kawaida uliohitimishwa
hivi karibuni, limewaandikia waamini na watu wote wenye mapenzi mema barua ya kichungaji
inayokazia dhamana ya Kanisa katika Uinjilishaji na tunu msingi za maisha ya kifamilia
nchini humo.
Maaskofu wanasema,
Uinjilishaji Mpya unalichangamotisha Kanisa kutafuta mbinu na mikakati mipya ya shughuli
za kichungaji ili kukabiliana kwa dhati na mmong’onyoko wa tunu msingi za maisha ya
kiutu, kiroho na kijamii katika familia nyingini nchini Vietnam.
Mwaka 2014,
Kanisa Katoliki nchini Vietnam litajikita zaidi katika Mikakati ya shughuli za Kichungaji
kwa ajili ya Familia. Wazo hili linakwenda sambamba na nia ya Baba Mtakatifu Francisko
ambaye ametangaza Maadhimisho ya Sinodi Maalum kuhusu Familia itakayofanyika mwezi
Oktoba, 2014 kwa kuongozwa na kauli mbiu “Changamoto za familia mintarafu Uinjilishaji”.
Maaskofu wanasema, Kanisa ni familia ya Mungu, Kanisa dogo la nyumbani na
kwamba, wongofu wa kweli unapata chimbuko lake kutoka katika familia. Huu ni mwaliko
kwa waamini kuhakikisha kwamba, wanajenga misingi itakayoiwezesha familia kuwa ni
shule ya sala, umoja, upendo na mshikamano unaodhihirisha ushuhuda wa imani katika
matendo kama sehemu ya mchakato wa Uinjilishaji wa Mpya.
Wazazi wanapaswa kutambua
dhamana na wajibu wao katika malezi kwani wao ndio walimu wa kwanza wa tunu msingi
za maisha ya kiroho, kiutu na kijamii. Watambue kwamba, familia bora za Kikristo ni
chemchemi ya miito mitakatifu ndani ya Kanisa. Familia goi goi, zinaweza kuzalisha
wahudumu wa Injili waliokengeuka kwa kukosa dira na mwelekeo sahihi katika maisha
kwani waswahili wanasema, samaki mkunje angali mbichi, akishakauka hakunjiki tena!
Baraza
la Maaskofu Katoliki Vietnam katika barua yake ya kichungaji linaendelea kukazia umuhimu
wa maandalizi ya kutosha kwa wanandoa watarajiwa, watakaoshiriki kwa ukamilifu maisha
na utume wa Kanisa, wakitambua kwamba, wanawajibika katika mchakato wa ujenzi wa Fumbo
la Kanisa, Jamii na Nchi yao katika ujumla wake. Kinzani na migogoro inayojitokeza
katika maisha ya ndoa na familia, ni mwaliko kwa Kanisa Katoliki nchini humo kuendelea
kufafanua maana ya ndoa kadiri ya Kanisa Katoliki, umuhimu na dhamana yake.
Jumuiya
za waamini zitambue familia zinazokabiliwa na matatizo na changamoto za maisha, ili
ziweze kuwasaidia kwa sala, mawazo na matendo, badala ya kuwalaani na kuwatenga kana
kwamba, wao ni mzigo katika maisha na utume wa Kanisa. Familia zenye matatizo, migogoro
na kinzani, zinapaswa kuonjeshwa upendo na moyo wa ukarimu.
Kutokana na mwelekeo
kama huu, Maaskofu Katoliki wa Vietnam wanapenda kukazia majiundo ya awali na endelevu
kwa Makleri, Watawa na Waamini walei wanaojihusisha kikamilifu katika kuwandaa wanandoa
watarajiwa.
Maaskofu katika mikakati yao ya kichungaji kwa Mwaka 2014 hadi
2016 watajikita katika dhamana ya Uinjilishaji wa Parokia na Jamii. Maaskofu wanahitimisha
barua yao ya kichungaji kwa kuwaomba Mashahidi wa Vietnam, ambao ni kielelezo makini
cha Uinjilishaji wa kina, wawasaidie waamini kuishuhudia imani yao kwa Kristo kwa
njia ya matendo.