2013-11-08 15:21:08

Zingatieni sura ya Mchungaji mwema, mnapotekeleza wajibu wa Kanisa kuinjilisha na kutoa haki!


Mahakama kuu ya Vatican inao wajibu wa kusaidia shughuli za kitume zinazofanywa na Makanisa mahalia katika mchakato wa kuhakikisha kwamba, haki ndani ya Kanisa inatendeka kwa kutoa maamuzi sahihi. Ni mahakama inayopaswa kushirikiana bega kwa bega na Maaskofu ili kuwawezesha kuwa kweli ni wahudumu wa amani.

Ubatilishaji wa ndoa za Kikristo ni kati ya kazi nyeti inayotekelezwa na Mahakama kuu ya Vatican; utume ambao unawataka wadau kutekeleza wajibu wao barabara, ili ukweli na haki viweze kutolewa kwa ajili ya mafao ya shughuli za kichungaji kwa pande zote zinazohusika. Mahakama hii imekwisha toa mchango mkubwa katika maisha na utume wa Kanisa, hasa zaidi katika maandalizi ya Hati ya Kichungaji "Dignitas Connubii", "Heshima ya Wanandoa" inayotoa sheria elekezi katika masuala ya ndoa.

Ni maneno ya Baba Mtakatifu Francisko alipokutana na wajumbe wa Mahakama kuu ya Vatican wanaofanya mkutano wao wa Mwaka kwa kuangalia kanuni na mikakati inayoweza kutumika kwa ajili ya kuimarisha mshikamano wa ndoa katika mchakato wa sheria za Kanisa mintarafu ubatilishaji wa ndoa.

Baba Mtakatifu anawataka wajumbe hawa kusimama kidete kulinda na kutetea mshikamano wa wanandoa; kwa kuhakikisha kwamba, wanatafuta ushahidi ili kuhakiki madai yanayoletwa mbele yao, kwa kuheshimu ukweli na mshikamano wa ndoa. Matatizo ya kiakili ni kati ya mambo yanayoweza kusababisha kuvunjika kwa ndoa, kumbe, wanapaswa kuwa makini katika mambo haya; kwa kusoma na kupitia mwenendo mzima wa kesi husika bila kushinikizwa na ukiritimba au masuala ya mpito! Wao wanapaswa kuwa ni wapatanishi kati ya Sheria za Kanisa, hali ya Kanisa na Jamii katika ujumla wake.

Wao kama watetezi wa sheria za Kanisa, wanayo dhamana ya kutoa maana ya kesi iliyoko mbele yao hata wakati mwingine kwa kukata rufaa kwenye Mahakama kuu ya Rufaa ya Vatican, pale inapoonekana kwamba, maamuzi yanakwenda kinyume cha ukweli dhidi ya mshikamano wa ndoa; mambo yanayohitaji ushirikiano wa dhati katika maboresha ya shughuli hizi.

Baba Mtakatifu anasema, Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican wanasema, Kanisa ni kielelezo cha umoja, kumbe hata mtetezi wa ndoa anapaswa kutekeleza wajibu wake kwa kuzingatia mwelekeo huu, kwa kuthamini, kuheshimu na kukuza majadiliano kati ya watu wanaohusika.

Baba Mtakatifu Francisko anawaambia wafanyakazi wa Kanisa wanaoshughulikia utume wa haki ya Kanisa, kutambua kwamba, wanafanya kazi hii kwa niaba ya Kanisa na kwamba, wao pia ni sehemu ya Kanisa, kumbe, kuna haja ya kuweka uwiano makini kati ya Kanisa linaloinjilisha na Kanisa linalotoa haki. Huduma ya kichungaji katika shughuli za haki ni dhamana ya kitume inayopaswa kutekelezwa kwa kuzingatia ile sura ya Mchungaji mwema anayejitaabisha kutafuta Kondoo aliyejeruhiwa na kupotea.

Mwishoni, Baba Mtakatifu anaendelea kuwatia moyo katika utekelezaji wa utume wao kwa kuwa waangavu na wenye haki ndani ya Kanisa, kama njia ya kupata majibu muafaka na shahuku ya waamini kwa viongozi wao wa Kanisa, ili waweze kufafanuliwa hali yao ya maisha.







All the contents on this site are copyrighted ©.