Umoja wa Makanisa hauna budi kusimikwa katika misingi ya Imani kwa Kristo na Kanisa
lake!
Maadhimisho ya Mkutano wa kumi wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni, (WCC), mjini Busana,
Korea ya Kusini, imekuwa ni fursa kwa wajumbe kuweza kufanya tafakari ya kina kuhusu
umoja wa Makanisa katika mambo matakatifu. tafakari hii imefanywa kwa kusukumwa zaidi
na moyo wa sala pamoja na kushirikishana maoni mintarafu mchakato mzima wa majadiliano
ya kiekumene, unaosukumwa na ile Sala ya Yesu, ili wote wawe wamoja.
Wajumbe
wamejadili kuhusu safari ya umoja wa Makanisa, matumaini na changamoto zake, kwa kutambua
kwamba, umoja ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwa ajili ya waja wake na mwaliko
endelevu kutoka kwa Kristo mwenyewe. Msingi wa umoja wa majadiliano ya kiekumene hauna
budi kujikita katika imani kwa Kristo na Kanisa lake. Umoja huu unapaswa kujipambanua
kwa mambo yanayoonekana kwa nje, lakini zaidi katika yale yanayofumbatwa katika undani
wa maisha ya Mkristo.