2013-11-08 09:17:10

"Shuhudieni huruma ya Mungu na mjikite barabara katika majiundo ya majandokasisi"!


Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe alioliandikia Baraza la Maaskofu Katoliki Ufaransa wakati huu wanapofanya mkutano wao wa Mwaka, mjini Lourdes, anawasihi kujitosa bila ya kujibakiza kwa ajili ya huduma kwa binadamu, lakini zaidi kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.

Anawataka kujikita zaidi katika majiundo ya Majandokasisi ili waweze kukita mizizi yao katika Kristo, tayari kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya Mungu na jirani zao. Baba Mtakatifu anaendelea kuwaalika Maaskofu Katoliki kuwa karibu zaidi na waamini waliokabidhiwa kwao na Kristo katika huduma za kichungaji.

Baba Mtakatifu katika ujumbe wake kwa Askofu mkuu George Pontier, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Ufaransa, anaishukuru Familia ya Mungu nchini humo kwa kukuza na kuimarisha ari na moyo wa kimissionari, hali inayojionesha kwa namna ya pekee katika Parokia za Kanisa Katoliki nchini Ufaransa. Waamini wanaalikwa kuendeleza mchakato wa toba na wongofu wa ndani kama ushiriki wao makini katika Uinjilishaji mpya unaodai ushuhuda wa imani tendaji.

Baba Mtakatifu anawashukuru pia Maaskofu kutoka sehemu mbali mbali za dunia wanaofanya mikutano yao kama kielelezo cha mshikamano wa Kiaskofu pamoja na Khalifa wa Mtakatifu Petro kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa la Kristo.







All the contents on this site are copyrighted ©.