Tanzania kuchangia askari katika Kikosi cha Afrika
Tanzania ni miongoni mwa nchi tano za Afrika ambazo zimejitolea kutoa askari wa kuunda
Kikosi cha Kukabiliana na Migogoro ya Kijeshi Barani Afrika cha African Capacity for
Immediate Response to Crises (ACIRC) kitakachoundwa kwa mujibu wa uamuzi wa Wakuu
wa Nchi Wanachama wa Umoja wa Afrika (AU). Tanzania itatoa kikosi kimoja (Battalion
Group) na nchi nyingine ambazo zimekubali kuchangia askari ama polisi katika Kikosi
hicho ni Afrika Kusini, Uganda, Algeria na Chad.
Nchi hizo zilijitokeza kushiriki
katika Kikosi hicho wakati wa Mkutano wa Wakuu wa Majeshi wa nchi hizo uliofanyika
Jumapili iliyopita mjini Pretoria, Afrika Kusini, mkutano ambao maamuzi yake yameidhinishwa
na kukubaliwa na wakuu wa nchi akiwamo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa
Jakaya Mrisho Kikwete. Wakuu hao walikutana Pretoria, Jumanne, Novemba 5, 2013.
Uamuzi
wa kuanzisha Kikosi hicho ulitolewa na Wakuu wa Nchi wanachama wa AU waliokutana katika
kikao chao cha 22 cha kawaida mwezi Mei, mwaka huu, 2013, mjini Addis Ababa. ACIRC
kitakuwa kikosi cha muda wakati Afrika inaendelea na maandalizi yake ya kuunda Jeshi
la Kudumu la Afrika (Africa Standby Force) na Lenye Uwezo wa Kukabiliana na Migogoro
Haraka na Popote (Rapid Deployment Force).
Jeshi hili litakuwa ni jeshi lenye
uwezo wa kuingia nchi yoyote, chini ya AU, na hivyo wakati mwingine litatumika kutuliza
migogoro katika nchi yoyote ya Afrika hata kama nchi husika haijaomba msaada wa jeshi
hilo. Jeshi hilo litakalofanya kazi yake chini ya mfumo wa Amani na Usalama katika
Afrika – African Peace and Security Architecture (APSA) litaiwezesha AU kuwa na jeshi
la askari na polisi wenye uwezo na nguvu kukabiliana na mizozo ya kijeshi barani humo
na kuwa vifaa vyake vitatolewa nchi wanachama wa AU ambao watakuwa tayari kushiriki
katika mpango huo.