2013-11-07 09:08:40

Komesheni kinzani, migogoro na vita ili watu wajikite katika mchakato wa maendeleo endelevu!


Viongozi Barani Afrika hawana budi kusimama kidete kulinda na kutetea haki msingi za binadamu, amani na utulivu sanjari na kuponya makovu ya chokochoko na kinzani za kidini, kisiasa na kijamii, ili kuzuia majanga yanayoendelea kujitokeza kwa wakimbizi na wahamiaji kutoka Barani Afrika kujikuta wanakufa maji, katika harakati za kutafuta usalama na ubora wa maisha ughaibuni!

Utawala bora, mikakati makini ya maboresho ya uchumi na maisha ya kijamii ni mambo msingi ambayo yanaweza kulisaidia Bara la Afrika kujinasua kutoka katika lindi la umaskini, magonjwa, njaa na vita. Huu ni mchango uliotolewa na wajumbe wa tume ya haki na amani kutoka Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu katoliki Afrika na Madagascar, SECAM katika mkutano wake wa Mwaka uliohitimishwa hivi karibuni mjini Bujumbura, Burundi.

Wajumbe hawa wanasema, kuna ongezeko kubwa la biashara haramu ya binadamu na viungo vyake kutoka Barani Afrika. Baadhi ya nchi bado zinaendelea kukabiliana na kinzani, migogoro na vita inayojikita katika masuala ya: ukabila, udini, uchu na uroho wa madaraka. Baadhi ya viongozi Barani Afrika wameendelea kufumbia macho chokochoko za kidini kwa baadhi ya waamini wenye misimamo mikali ya kidini kufanya mashambulizi dhidi ya raia wengine, bila ya kufikishwa kwenye mkondo wa sheria. Haya ndiyo yanayojitokeza nchini Nigeria, Mali, Misri, Somalia, Kenya na Tanzania.

Kuna baadhi ya viongozi wa Serikali wanashirikiana na makampuni makubwa kutoka ndani na nje ya Bara la Afrika kwa ajili ya kunyonya utajiri na rasilimali ya Afrika kwa ajili ya mafao ya watu wachache, wakati kundi kubwa la raia wakiendelea kuogelea katika dimbwi la ujinga, umaskini na maradhi. Wajumbe hao wanaitaka Mamlaka ya Bonde la Mto Nile, kutambua kwamba, kuna mamillioni ya watu yanategemea ustawi, maisha na maendeleo yao kutokana na maji ya Mto Nile, kumbe maamuzi yoyote yanapaswa kuzingatia kwanza mafao ya wengi kwa njia ya majadiliano ya kina!







All the contents on this site are copyrighted ©.