2013-11-07 09:41:06

Jitoeni kimasomaso kulinda na kutetea misingi ya haki, amani na utulivu!


Wajumbe wa mkutano mkuu wa kumi wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni wameendelea kujadili pamoja na mambo mengine, kuhusu umuhimu wa kusimama kidete kulinda na kutetea na kudumisha misingi ya haki na amani duniani. Itakumbukwa kwamba, mkutano huu unaongozwa na kauli mbiu "Mungu wa uhai, tuongoze katika misingi ya haki na amani.

Haki inayotafutwa inapaswa kujidhihirisha katika medani mbali mbali za maisha ya mwanadamu: kwa mfano katika sekta ya uchumi, fedha na biashara kwa kuhakikisha kwamba, wadau wanawajibika kutoa kipaumbele cha kwanza kwa utu, heshima na maisha ya mwanadamu. Makanisa hayana budi kuwezeshwa kikamilifu ili kupambana na majanga katika maisha ya mwanadamu pamoja na kutunza mazingira.

Maadili ya kazi na utume wema ni kati ya vipaumbele vinavyokaziwa na wajumbe wa mkutano mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni huko Busan, Korea ya Kusini. Kufilisika kwa Mabenki na Makampuni makubwa kutoka Ulaya na Amerika ni chanzo kikubwa cha athari za myumbo wa uchumi kimataifa unaoendelea kusababisha majanga kwa mamillioni ya familia duniani, kiasi kwamba, hata wale wanaoishi katika nchi zinazoendelea sasa wanaanza kuonja makali ya athari za myumbo wa uchumi kimataifa.

Jamii inapaswa kuwaangalia wanyonge na watu wenye ulemavu, kama sehemu ya mchakato wa kulinda na kutetea zawadi ya uhai kutoka kwa Mwenyezi Mungu na kwamba, vijana wapewe fursa za ajira ili waweze kukabiliana na maisha kikamilifu. Makanaisa yaendelee kuwa mstari wa mbele katika mapambano dhidi ya uvunjifu wa haki msingi za binadamu, dhuluma, nyanyaso na ubaguzi wa rangi. Makampuni makubwa yanayowekeza vitega uchumi vyake katika nchi changa zaidi duniani yasaidia kuchangia mchakato wa maendeleo endelevu na maboresho ya maisha ya watu katika elimu na afya.

Jumuiya ya Kimataifa inapaswa kutambua kwamba, upendo ni chemchemi ya haki, amani, utulivu na maendeleo. Watu wanapaswa kujenga na kuimarisha mapendo kati yao na mazingira, ili dunia iweze kuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi. Huduma bora za afya ni sehemu ya haki, Serikali na wadau mbali mbali wahakikishe kwamba, haki hii inawafikia watu wengi zaidi badala ya kujikita kutafuta faida kubwa kwa gharama ya maisha ya watu wanyonge!

Wajumbe wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni wanatambua na kuheshimu mchango wa wanawake Wakristo katika ustawi na maendeleo ya Makanisa ulimwenguni. Wanataka wanawake hawa wawezeshwe kwa hali na mali ili waendelee kuchangia zaidi katika maendeleo ya Makanisa mahalia. Kuna haja ya kuendelea kuhimiza mikakati ya kilimo cha kisasa na utunzaji bora wa mazingira, ili kupambana na athari za mabadiliko ya tabianchi.







All the contents on this site are copyrighted ©.