2013-11-07 07:55:44

Bagamoyo ni ishara ya moyo uliopondeka na kuvunjika; kielelezo cha mwanga na matumaini mapya katika Kristo!


Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania linapojiandaa kwa ajili ya Maadhimisho ya Kufunga Mwaka wa Imani, hapo tarehe 10 Novemba 2013 mjini Bagamoyo, Askofu mkuu Josephat Lebulu wa Jimbo kuu la Arusha katika mahojiano na Radio Vatican anasema kwamba, mji wa Bagamoyo ni kielelezo cha moyo uliopondeka na kuvunjika kutokana na dhuluma, nyanyaso na madhara makubwa ya biashara ya utumwa duniani. RealAudioMP3

Bagamoyo ni Mlango wa Imani kwa Kanisa la Afrika Mashariki, kwani Wamissionari wa kwanza kujitosa kimasomaso kutangaza Habari Njema ya Wokovu walitua nanga ya matumaini ya watu mjini Bagamoyo. Hapa mwanadamu akapata matumaini na mwanga mpya wa maisha, kiasi cha kuanza kutembea katika uhuru na mwanga wa Kristo Mfufuka. Bagamoyo ukageuzwa na kuwa ni kielelezo cha maisha mapya katika Kristo na kinzani katika hija ya imani.

Askofu mkuu Lebulu anasema kwamba, Bagamoyo imekuwa ni ishara ya upinzani na tumaini jipya; mwanga mpya wa maisha badala ya kukata tamaa. Licha ya Bagamoyo kuwa ni Mlango wa Imani ya Kikristo, lakini bado mji huu umebaki nyuma katika maisha ya Kikristo, lakini watu wameufahamu mpango wa Mungu unaopania kuwakomboa wote! Kumbe, Bagamoyo unabaki kuwa ni Mlango wa Imani na Mwanga wa matumaini mapya.







All the contents on this site are copyrighted ©.