2013-11-06 10:36:44

Biashara haramu ya binadamu inaongezeka kwa kasi nchini Uingereza!


Wadau wanaopambana dhidi ya biashara haramu ya binadamu kutoka Uingereza wanasema kwamba, biashara hii pamoja na biashara haramu ya viungo vya binadamu inaendelea kushamiri katika nchi zinazoendelea duniani kutokana na uchu wa mali na utajiri wa haraka haraka.

Kuna baadhi ya watu ndani ya Jamii wanatumia umaskini wa wananchi kwa ajili ya kuwarubuni na hatimaye, kuwatumbukiza katika biashara haramu ya binadamu. Vyombo vya ulinzi na usalama nchini Uingereza vinaendelea kufanya uchunguzi wa kina kuhusiana na kundi la watu linalojihusisha na biashara haramu ya binadamu. Inasemekana hivi karibuni, mtoto aliyetekwa nyara kutoka Somalia, alikamatwa nchini Uingereza, akiwa kwenye mchakato wa kunyofolewa viungo vyake ili viweze kuuzwa kwenye soko la magendo!

Mashirika yasiyo ya kiserikali yanayoongoza mapambano dhidi ya biashara haramu ya watoto, picha za ngono na utalii wa ngono wanasema, mambo haya yananyanyasa na kudhalilisha utu na heshima ya watoto hawa na kwamba, vitendo hivi vinaendelea kuongezeka kwa kasi kubwa nchini Uingereza. Takwimu zinaonesha kwamba, ongezeko hili limefikia asilimia 50% tangu mwaka jana. Jeshi la Polisi Uingereza linasema kwamba, watoto 371 wametumbukizwa katika utalii wa ngono. Wengi ya watoto hawa ni wale wanaotoka Vietnam, Nigeria, China, Romania na Bangaladesh. Idadi hii inachafuliwa pia na uwepo wa watoto 20 kutoka Uingereza.







All the contents on this site are copyrighted ©.