2013-11-05 07:39:35

Wosia kwa wasomi!


Wanafunzi wanaotumwa na Maaskofu, Wakuu wa Mashirika na Vyama vya Kitume kuja Roma ili kujinoa wanapaswa kutambua kwamba, wao ni wawakilishi wa Kanisa la Afrika, wametumwa ili kunoa akili zao, tayari kulitumikia Kanisa la Afrika kadiri ya mpango wa Mungu katika maisha yao na wala si vinginevyo. RealAudioMP3

Wosia huu umetolewa na Mheshimiwa Padre Alcuini Nyirenda, OSB wakati wa hafla ya kuwakaribisha Wanafunzi Wakatoliki kutoka Tanzania waliofika hivi karibuni tayari kuanza safari ya maisha ya ughaibuni, hapo tarehe 3 Novemba 2013, kwa ajili ya kujipatia ujuzi, maarifa na stadi za maisha. Wanafunzi wamekumbushwa kutambua kwamba, wao ni tegemeo la Kanisa Barani Afrika kwa sasa na kwa siku za usoni.

Muda wa masomo, kiwe ni kipindi cha kujifunza kwa bidii, juhudi na maarifa, lakini wasiwe na matumaini makubwa katika maisha kwa kudhani kwamba, baada ya masomo yao, basi watakuwa "watu fulani katika Kanisa na Jamii katika ujumla wake". Mawazo kama haya yatawafanya waendelee kuwa wafupi wa kimo kama ilivyokuwa kwa Zakayo mtoza ushuru anayesimuliwa katika Injili ya Jumapili iliyopita.

Padre Nyirenda amewakumbusha wanafunzi hawa kwamba, wanapohitimu masomo yao na kurudi nyumbani, watambue kwamba, Kanisa lina malengo na mikakati yake ya shughuli za Uinjilishaji, kumbe malengo binafsi yasiwe ni kikwazo kwa lengo kuu ambalo linapata chimbuko lake kutoka kwa Mungu mwenyewe. Jambo la msingi kwa sasa ni kuhakikisha kwamba, wanajitosheleza wenyewe katika ukweli na utumilifu wa maisha yao kama binadamu. Kila mtu ajitambue na kujitahidi kuwa mwenyewe! Ni mwaliko wa kuonesha ukomavu katika maisha, Mwenyezi Mungu akipewa kipaumbele cha kwanza.

Wasomi wanatakiwa kushirikiana na Mwenyezi Mungu katika mchakato wa kumletea mwanadamu ukombozi wa kweli na maendeleo endelevu yanayogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili. Daima katika maisha yao wajitahidi kumwilisha, upendo kwa Mungu na jirani, hii ndiyo kanuni msingi kwa ajili ya mafanikio katika maisha ya kila mwamini.







All the contents on this site are copyrighted ©.