Upendo kwa Mungu na jirani ndiyo lugha inayokoleza mchakato wa Uinjilishaji Mpya!
Askofu mkuu Antonio Ariotti, Balozi wa Vatican nchini Paraguay katika hotuba yake
kwenye mkutano wa 198 wa Baraza la Maaskofu Katoliki Paraguay, amelishukuru Kanisa
Katoliki Amerika ya Kusini, kwa kulizawadia Kanisa la kiulimwengu Baba Mtakatifu Francisko
ambaye kwa sasa, anajitahidi kuendeleza mchakato wa Uinjilishaji mpya kwa njia ya
maisha, maneno na matendo yake yanayogusa sakafu ya mioyo ya watu wengi duniani.
Mama
Kanisa bado anaendelea kuchangamotishwa na Kristo kuubeba Msalaba kama kielelezo cha
huruma na upendo wa Mungu kwa waja wake katika hija ya kuwatangazia watu Habari Njema
ya Wokovu sanjari na kuwaimarisha waamini katika imani yao kwa Kristo na Kanisa lake.
Huu ni mwendelezo wa Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, uliotangazwa na kuzinduliwa na
Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, ukaendelezwa na Papa Francisko kwa
ari na moyo mkuu!
Mwaka wa Imani, kimekuwa ni kipindi cha kugundua tena na
tena zawadi ya imani kutoka kwa Mwenyezi Mungu, ili iweze kuwa ni taa na dira inayomwangazia
mwanadamu katika maisha na vipaumbele vyake kwa njia ya maneno, lakini kwa kujikita
zaidi katika matendo ya huruma, kielelezo makini cha imani tendaji kwa maskini na
wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Upendo kwa Mungu na jirani ndiyo lugha inayokoleza
mchakato wa Uinjilishaji Mpya.
Askofu mkuu Antonio Ariotti amelipongeza Baraza
la Maaskofu Katoliki Paraguay kwa kujiwekea mikakati ya maisha na utume wa Kanisa
katika kukuza na kudumisha misingi bora ya maisha ya ndoa na familia, mwelekeo unaokwenda
sanjari na nia ya Baba Mtakatifu Francisko katika kuitisha Sinodi Maalum ya Maaskofu
itakayojadili changamoto za kichungaji katika mchakato wa Uinjilishaji Mpya, Sinodi
ambayo itaadhimishwa Mwezi Oktoba 2014.
Anasema, Paraguay inapaswa kujiwekea
mikakati na mbinu makini zitakazowasaidia wananchi kushiriki kikamilifu katika mchakato
wa maboresho katika sekta ya elimu, afya, maendeleo endelevu, amani na utulivu. Ni
dhamana ya Maaskofu kuwajengea waamini na wananchi uwezo wa kufanya majadiliano ya
kina kwa ajili ya mafao ya wengi; lakini zaidi katika mapambano dhidi ya umaskini,
ujinga na maradhi; wananchi hawana budi kusimama kidete kupinga kwa nguvu zao zote
mambo yanayopelekea ukosefu wa amani, utulivu na usalama kwa kuzingatia utawala wa
sheria.
Wananchi wanapaswa kupambana kufa na kupona dhidi ya mambo yote yanayopelekea
ukosefu wa haki msingi za kijamii; rushwa na ufisadi; ubaguzi na ukosefu wa fursa
za ajira miongoni mwa vijana. Baraza la Maaskofu Katoliki Paraguay linaendelea kuufanyia
kazi ujumbe wa Baba Mtakatifu Francisko aliowapatia Maaskofu wa Amerika ya Kusini
kuhusu mwelekeo wa Kanisa kwa siku za usoni. Wanajadili pia mambo msingi katika maisha
na utume wa Kanisa nchini humo.