Mnaalikwa kwenye Karamu ya Bwana! Wakristo msiridhike kuwa katika orodha ya wageni
waalikwa! Mnatakiwa kufanya makubwa zaidi!
Baba Mtakatifu Francisko katika Maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kikanisa
cha Mtakatifu Martha, Jumanne, tarehe 5 Novemba 2013 anawaalika waamini kuhakikisha
kwamba, wanasherehekea kikamilifu Karamu ya Bwana. Wakristo watambue kwamba, wanaalikwa
na Mwenyezi Mungu kushiriki karamu hii wakiwa na dhamiri safi na nyofu.
Karamu
ya Bwana ni sherehe inayobubujika furaha, matumaini na mapendo kutoka kwa Kristo;
sherehe ambayo inawakumbatia wote pasi na ubaguzi kwani wao ni sehemu ya viungo vya
Fumbo la Mwili wa Kristo, yaani Kanisa, kila mtu ana wajibu na dhamana ya kutekeleza
kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa. Wakristo wajitambue kwamba, wao ni sehemu
muhimu sana ya Kanisa la Kristo! Karamu hii ni mwaliko wa kujenga na kudumisha umoja
miongoni mwa Wakristo, kila mwamini akijitahidi kujitakatifuza kwa nyenzo mbali mbali
zinazotolewa na Mama Kanisa.
Baba Mtakatifu Francisko anasema kwamba, Kanisa
linawakumbatia watakatifu na wadhambi; na kwamba, kila mmoja wao ana karama na zawadi
ambayo amekirimiwa na Roho Mtakatifu; zawadi ambayo anapaswa kuifanyia kazi barabara
kwa ajili ya mafao ya Kanisa. Kanisa linapaswa kuwakumbatia wote kwa kuanzia na wale
wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.
Inasikitisha kuona kwamba, kuna baadhi
ya Wakristo wamepewa mwaliko na wako kwenye orodha ya waalikwa, lakini bado wanagoma
kuhudhuria Sherehe ya Mwanakondoo wa Mungu kwa visingizio kibao! Wanashindwa kutambua
kwamba, kuingia ndani ya Kanisa ni mwaliko na neema inayowataka waamini kujenga na
kuimarisha Jumuiya ya Kikristo, kila mtu akitumia kikamilifu karama na vipaji vyake
kwa ajili ya Kanisa na Jirani zake. Kristo anaendelea kuwaalika waamini kufanya hija
inayowapeleka kwenye maisha ya uzima wa milele na kwamba, Mwenyezi Mungu ndiye kiongozi
mkuu wa safari hii ya maisha ya kiroho.
Baba Mtakatifu anasema, Yesu ni mwingi
wa huruma na mapendo, hata kwa wale wanaoonesha shingo ngumu kwa mwaliko wake. Anaendelea
kuwasubiri kwa saburi na mapendo makuu. Yesu anawapenda watu ambao ni wanyofu na wa
kweli katika maisha yao: kwa maneno na matendo.
Inapendeza ikiwa kama Wakristo
wote wataweza kushiriki katika Karamu ya Bwana, ili kuonja furaha inayobubujika kutoka
kwa Kristo na wala wakristo wasiridhike kwamba, majina yao yameandikwa kwenye orodha
ya waalikwa kwenye Karamu ya Bwana, bali wanatakiwa kushiriki bila kutoa visingizio!