2013-11-05 07:23:21

Majadiliano ya kidini ni muhimu katika kulinda, kukuza na kutetea haki msingi za binadamu, amani na mshikamano wa kitaifa!


Visiwa vya Zanzibar ni mlango wa Imani ya Kanisa Katoliki Afrika Mashariki. Hii inatokana na juhudi zilizofanywa na Wamissionari wa Roho Mtakatifu yapata miaka 150 iliyopita. RealAudioMP3
Juhudi za Wamissionari hawa zilipania pamoja na mambo mengine kukomesha biashara ya utumwa sanjari na kuwajengea wananchi uwezo wa kupambana na mazingira yao kwa njia ya elimu.
Majadiliano ya kidini kati ya Waislam na Wakristo Visiwani Zanzibar ni jambo la kihistoria tangu wakati wa utawala wa Sultan Sayyid Barghash aliyeruhusu ujenzi wa Kanisa katika eneo la Mji Mkongwe, Kanisa la Minara miwili. Waamini wa dini ya Kiislam na Kikristo waliishi pamoja na kuheshimiana kama ndugu hata katika tofauti za imani na tamaduni zao.
Askofu Augustino Shao wa Jimbo Katoliki Zanzibar anasema, hali ya amani, utulivu na uhuru wa kuabudu vinaanza kumong’onyoka taratibu Visiwani Zanzibar kutokana na kuibuka kwa chuki za kidini zinazofanywa na waamini wenye misimamo mikali ya kiimani. Chuki na uhasama huu kama havitaweza kudhibitiwa kikamilifu na vyombo vinavyohusika, maafa yake ni makubwa. Kumbe, kuna haja ya kuendeleza utamaduni wa majadiliano ya kidini, hali ya kuvumiliana, kuheshimiana na kusaidiana kama ndugu bila ya kuwepo kwa misingi ya ubaguzi unaoendekezwa kwa misingi ya udini. Waislam na Wakristo ni wakazi wa Zanzibar na wote wana haki ya kuendelea kuishi Zanzibar.
Askofu Shao anasema kwamba, chuki za kidini na ubaguzi dhidi ya Wakristo ni jambo ambalo limepandikizwa, kwa ajili ya mafao ya watu wachache wasiowatakia mema wananchi wa Zanzibar katika ujumla wao. Hakuna uhusiano wowote kati ya Muungano na Kanisa; kwani siasa zinafanywa na wanasiasa na Kanisa linahubiri Habari Njema ya Wokovu, mambo mawili tofauti kabisa! Madhulumu ya viongozi wa Kanisa katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani Visiwani Zanzibar imekuwa ni changamoto kubwa kwa waamini kusimama kidete kulinda, kutetea na kushuhudia imani yao kwa Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu!
Ubaguzi na madhulumu ya kidini yasipodhibitiwa kwa ukamilifu, Zanzibar inaweza kujikuta ikitumbukia katika maafa na kuharibu jina zuri la Visiwa vya Zanzibar katika ramani ya dunia. Watu wachache wenye nia mbaya wasiruhusu kuvuruga amani, upendo na mshikamano wa kitaifa Zanzibar.
Watu wajenge moyo na utamaduni wa kujadiliana, kuheshimiana, kuthaminiana na kusaidiana. Uhuru wa kidini ni kati ya haki msingi za binadamu, uheshimiwe na kulindwa na vyombo husika. Matukio ya kuchomwa moto kwa Makanisa, kushambuliwa kwa viongozi wa kidini ni kati ya mambo yanayoendelea kuwatia hofu wananchi wengi Visiwani Zanzibar. Mwaka wa Imani iwe ni fursa ya kuimarisha imani, matumaini na mapendo miongoni mwa waamini na watu wote wenye mapenzi mema Visiwani Zanzibar.








All the contents on this site are copyrighted ©.