2013-11-04 12:12:17

Mkate, akili, elimu na umaskini ni tema zinazokwenda pamoja katika maisha ya mwanadamu!


Kardinali Peter Turkson, Rais wa Baraza la Kipapa la haki na amani katika hotuba yake ya ufunguzi wa mkutano wa Kikosi kazi cha Baraza la Kipapa la Taasisi za Sayansi, Jumatatu tarehe 4 Novemba 2013 anabainisha kwamba, "Mkate, Akili, Elimu na Umaskini" ni mambo yanayokwenda pamoja, kiasi cha kuwatumbukiza mamillioni ya watu katika lindi la umaskini, ujinga, njaa na utapiamlo wa kutisha

Mwili unaopata lishe bora unakuwa na afya njema ya akili na roho na kwamba, elimu ni chakula cha akili ya mwanadamu. Mada zinazojadiliwa na kikosi kazi katika mkutano wake zinarandana na Malengo ya Maendeleo ya Millenia, ifikapo Mwaka 2015; yanayopania pamoja na mambo mengine kuhakikisha kwamba, Jumuiya ya Kimataifa inafutilia mbali umaskini, ujinga na baa la njaa na kwamba, watoto wengi zaidi wanapata fursa ya elimu ya msingi. Watoto wanaopata chakula shuleni wameonesha mafanikio makubwa katika sekta ya elimu katika nchi zinazoendelea duniani.

Kardinali Turkson anasema kwamba, kuna haja kwa akili na mwili kulishwa vyema kwa njia tafiti makini za kisayansi sanjari na matumizi bora ya sayansi na teknolojia itakayomwezesha mwanadamu kuzalisha chakula na lishe ya kutosha pamoja na kumjengea mwanadamu uwezo wa kupambana na baa la umaskini duniani, kama njia ya kuinua utu na heshima ya binadamu, kwani haya ni mambo yanayogusa haki, amani na utulivu kama ambavyo alikwisha wahi kusema Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita.

Lishe duni ya akili na mwili ni hatari kubwa kwa maisha ya mwanadamu; jambo linalopaswa kushughulikiwa kisayansi pamoja na sera makini zinazolenga maboresho katika sekta ya elimu, usalama na uhakika wa chakula kwa kuzingatia: uzalishaji, usambazaji pamoja na kuweka mikakati ya kilimo bora na endelevu; kwa kuongozwa na kanuni ya mshikamano na udugu.

Mchakato huu unahitaji majadiliano ya kina, ili kila upande uweze kuchangia mawazo na mikakati yake kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya binadamu. Majadiliano yatumike kubainisha vikwazo na vizingiti katika mapambano dhidi ya baa la njaa, umaskini na ujinga duniani ili kujenga mshikamano wa kidugu! Kila mwamini anachangamotishwa na Mama Kanisa kuhakikisha kwamba, anashiriki kikamilifu katika mapambano dhidi ya baa la njaa ili kila mtu aweze kupata riziki yake ya kila siku.

Waamini na watu wenye mapenzi mema, wasimame kidete kulinda na kutetea haki msingi za maskini pamoja na kushiriki katika ujenzi wa Jamii inayosimikwa katika misingi ya haki na amani.







All the contents on this site are copyrighted ©.