2013-11-04 09:34:23

Kituko cha Zakayo tajiri na fisadi ni kielelezo cha toba na wongofu wa ndani, ili kukumbatia amani, furaha na wokovu!


Umati mkubwa wa waamini na mahujaji kutoka sehemu mbali mbali za dunia, Jumapili iliyopita, tarehe 3 Novemba 2013 walikusanyika kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro ili kusali na kutafakari pamoja na Baba Mtakatifu Francisko, wakati wa Sala ya Malaika wa Bwana.

Baba Mtakatifu anasema, sehemu ya Injili ya Jumapili ya 31 ya Mwaka wa C wa Kanisa, inaonesha sehemu ya mwisho ya hija ya maisha na utume wa Yesu hapa duniani, inayopania kuwaokoa wanakondoo wa nyumba ya Israel waliopotea, utume unaoendelea kumwongezea maadui. Mwinjili Luka, anamwonesha Zakayo, tajiri na mkuu wa watoza ushuru; fisadi na mwizi wa kodi. Haya ni kati ya mambo yaliyopelekea Zakayo kushindwa kumwona Yesu uso kwa uso, kiasi cha kuparamia na kukwea juu ya mti ili aweze kumwona Yesu.

Yesu anapofika mahali pale, anayainua macho yake na kumwambia Zakayo ashuke upesi kwani Yesu alitamani kukaa naye nyumbani mwake. Yesu anamwita Zakayo kwa jina yule ambaye alionekana mfupi wa kimo kuliko wote, mtu ambaye alikuwa haonekani, lakini mbele ya Yesu anapata kipaumbele cha pekee! Huyu ndiye Zakayo, maana yake, "Mungu anakumbuka". Yesu anaamua kuingia na kukaa nyumbani kwa Zakayo, hali inayozua chuki na uhasama kati ya watu kwa kumshutumu Yesu kwamba, alikuwa anakaa na kula na wadhambi.

Baba Mtakatifu anasema, uwepo wa Yesu nyumbani kwa Zakayo unaleta: amani, furaha na wokovu. Hii ni kumbukumbu hai ya huruma na upendo wa Mungu kwa wadhambi na hakuna dhambi au tendo ambalo linaweza kufutilia mbali huruma na upendo wa Mungu kwani wao wameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Daima anaendelea kusubiri kwa uvulimivu kuwaona watoto wake wakimrudia kwa toba na wongofu wa ndani, ili aweze kuwaonjesha upendo na huruma yake isiyokuwa na kifani.

Kitendo cha Zakayo tajiri na mkuu wa watoza ushuru kinawashangaza wengi, lakini ni kielelezo cha wokovu, changamoto na mwaliko kwa kila mwamini kuchunguza dhamiri yake mbele ya Mwenyezi Mungu, ili kuonja uwepo endelevu wa Mungu katika hija ya maisha yake, Mungu ambaye yuko tayari kuwapokea na kuwakumbatia kama alivyofanya Yesu kwa Zakayo mtoza ushuru. Yesu mwingi wa huruma na mapendo, daima yuko tayari kusamehe na kusahau; bado anaendelea kuwaita watu kwa majina, jambo la msingi na kusikiliza kwa makini sauti yake na kuipokea kwa moyo wa furaha.

Kwa njia ya Kristo hata mdhambi aliyejikatia tamaa anaweza kutubu na kumwongokea Mungu; anaweza kumwokoa mwamini kutoka katika ubinafsi wake na kumkirimia zawadi ya upendo! Baba Mtakatifu alihitimisha tafakari yake kwa kuwasalimia na kuwatakia wote kheri na baraka zake za kitume.







All the contents on this site are copyrighted ©.