2013-11-04 10:14:01

Kikosi kazi cha Baraza la Kipapa la Taasisi za Kisayansi chaanza mkutano wake unaoongozwa na kauli mbiu "Mkate na Akili"


Baba Mtakatifu Francisko, Jumatatu tarehe 4 Novemba 2013 amekutana na washiriki wa mkutano wa kikosi kazi cha Baraza ya Kipapa la taasisi za Kisayansi na kupiga nao picha kwenye makazi yake ya muda ya Hosteli ya Mtakatifu Martha, mjini Vatican. Mkutano wa Kikosi kazi unatarajiwa kufungwa hapo tarehe 6 Novemba 2013.

Baraza hili la kipapa linautajiri mkubwa wa historia ya mikutano inayounganisha mabaraza na taasisi mbali mbali za kipapa, ili kuweza kujadili changamoto zinazojitokeza katika ulimwengu wa utandawazi mintarafu elimu na umaskini wa watu. Lengo la mkutano wa kikosi kazi ni kuibua mbinu mkakati utakaotumiwa na wengi katika mchakato wa maboresho ya maisha ya mwanadamu, ili kumwongezea matumaini zaidi.

Mkutano huu unaongozwa na kauli mbiu "Mkate na Akili", kwa kufanya rejea inayogusa maendeleo ya sayansi na teknolojia ili kuleta maboresho ya chakula na lishe sanjari na mapambano dhidi ya baa la njaa na utapiamlo; mambo ambayo yanachangia kwa kiasi kikubwa kuporomoka kwa ubora wa elimu hususan katika nchi zinazoendelea duniani.

Jumuiya ya Kimataifa imepiga hatua kubwa katika maendeleo ya sayansi na teknolojia, mambo yanayoweza kusaidia katika mapambano dhidi ya baa la njaa na lishe duni sanjari na maboresho ya sekta ya elimu kwa mamillioni ya watu katika nchi zinazoendelea duniani, ili kuinua utu na heshima yao; tayari kushiriki katika mikakati ya kujiletea maendeleo endelevu.

Kikosi kazi, kimegawanyika katika makundi makuu manne yanayopembua vinasaba vya mimea, ukuaji wa akili ya mwanadamu, usalama wa chakula na elimu kama sehemu ya mchakato wa ukuaji wa mtui mzima: kiroho na kimwili pamoja na kuangalia changamoto za kimaadili zinazoendelea kujitokeza.







All the contents on this site are copyrighted ©.