Kilele cha Mwaka wa Imani Tanzania, Bagamoyo kufunika!
Maadhimisho ya Mwaka wa Imani nchini Tanzania limekuwa ni tukio ambalo limeasidia
kukuza na kuimarisha imani ya waamini kwa Kristo na Kanisa lake. Waamini katika ngazi
mbali mbali wamefanya tafakari ya kina kuhusu: Fumbo la Msalaba, Sakramenti za Kanisa
na umuhimu wake, Maisha ya Sala na Ushuhuda wa maisha ya Kikristo kama kielelezo makini
cha imani tendaji.
Maadhimisho
ya Mwaka wa Imani nchini Tanzania yanakwenda sanjari na Jubilee ya Miaka 150 ya Ukristo
nchini Tanzania. Katika kipindi chote hiki Kanisa Katoliki limejikita katika Uinjilishaji
unaogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili. Mheshimiwa Padre Patern Patrick
Mangi, Katibu mtendaji Idara ya Liturujia ya Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania
katika mahojiano maalum na Radio Vatican anafafanua kuhusu mikakati ya Maaskofu Katoliki
Tanzania katika kufunga Mwaka wa Imani huko Bagamoyo.
Maadhimisho haya yataanza
hapo tarehe 8 Novemba 2013 na kilele cha Maadhimisho ya Kufunga Mwaka wa Imani nchini
Tanzania ni hapo tarehe 10 Novemba 2013, ili kutoa nafasi kwa Familia ya Mungu Majimboni,
kushiriki na Baba Mtakatifu Francisko katika kuufunga rasmi Mwaka wa Imani wakati
wa Sherehe za Kristo Mfame wa dunia. Familia ya Mungu itapata nafasi ya kutafakari
mada mbali mbali zilizoandaliwa na Maaskofu Katoliki Tanzania.