2013-11-02 09:10:53

Kila mmoja anapaswa kutua vyema Nanga ya moyo wake mahali pazuri panapofaa..


Papa Francisko Ijumaa jioni aliongoza Ibada ya Misa, akiwa katika lango la Makaburi ya Verano Roma, kwa ajili ya Maadhimisho ya Siku ya Watakatifu wote, na baadaye kuwaombea wahamiaji marehemu wote waliofariki jangwani au baharini, wakati wakiwa katika harakati za kutafuta maisha mapya.
Ibada hii ya Misa ya Kipapa ilifanyika katika eneo hilo la Makaburi ya kihistoria kwa jiji la Roma, baada ya kupita miaka 20 tangu Papa Yohane Paulo II alipofanya ibada kama hiyo Novemba Mosi, 1993.
Papa Francisko katika hotuba yake alisema, “mawazo yetu na yawaendee wale walio tutangulia na ambao sasa wako mbinguni pamoja na Bwana. Papa alionyesha imani yake kwamba wapo kwa sababu waliokolewa na Kristo . Na si tu waliokolewa kwa sababu ya matendo yao mema, lakini ni kutokana na imani yao kwa Kristu iliyowawezesha kuyafuata maagizo ya Mwokozi wao na kumpenda.

Mahali hapo Papa alikumbusha wote kwamba, tunaweza tu kuingia katika mlango wa mbinguni kwa damu yake Kristo. Ni Yeye ndiye atakaye tuhukumu na ndiye atakaye fungua mlango wa mbinguni. Hili ni tumaini letu, aliendelea, iwapo tutaendelea kutembea katika njia ya Kristo, tukidumu katika tumaini hili na kukubali kuandamana naye, naye kamwe hawezi kututelekeza.

Papa alieleza na kuwakumbuka Wakristu wa mwanzo ambao waliliweka tumaini kuwa nguzo ya maisha yao. Tumaini la moyo, ,lililosimikwa katika nanga ya wapendwa wetu waasisi , ambao sasa ni Watakatifu wako mahali ambako Kristo yuko na ambapo Mungu yuko. Hili ndilo tumaini letu alisisitiza Papa Francisko.

Kila mmoja wetu katika siku hizi , Papa aliendelea, anapaswa kufikiri juu ya mwisho wa maisha yake. Ni lazima kuangalia mbele kwa matumaini na furaha ya kupokelewa na Bwana.Ni lazima tujiulize , mahali tulipoweka nanga ya moyo wetu , na kuhakikisha kwamba nanga hiyo imetua vizuri katika pwani ya maisha .

Papa alikamilisha ibada hii kwa kuwakumbuka Marehemu wote waliofariki jangwani au bahari wakati wakihangaika kutafuta njia mpya za kuwa na maishayaliyo bora zaidi.







All the contents on this site are copyrighted ©.