2013-11-01 12:10:16

Sekretarieti ya Papa itakuwa na uwezo wa kumsaidia Khalifa wa Mtakatifu Petro kutekeleza wajibu wake kwa Kanisa la Kristo!


Askofu mkuu Pietro Parolin amerejea mjini Roma, tayari kwa maandalizi ya utume wake mpya kama Katibu mkuu wa Vatican dhamana aliyopewa na Baba Mtakatifu Francisko kwa mshangao mkubwa na bila hata masitahili yake. Anasema, ameanza maisha haya mapya, taratibu, ingawa anakiri kwamba, walau anao uzoefu na mang'amuzi ya utume huu mpya kwani aliwahi kufanya kazi kwenye Sekretarieti ya Vatican kabla ya kuteuliwa kuwa Balozi wa Vatican nchini Venezuela.

Askofu mkuu Parolin mwenye umri wa miaka 58 anasema, kunako mwaka 1992 aliteuliwa kufanya kazi kwenye Sekretarieti ya Vatican, sehemu ya pili. Mwaka 2000 alihamishiwa kwenye kitengo cha mashauri ya kichungaji kwa watawa na wahudumu wa maisha ya kiroho magerezani na hospitalini. Kunako mwaka 2002 akateuliwa kuwa ni Katibu mkuu msaidizi wa mambo ya nchi za nje na ushirikiano wa kimataifa mjini Vatican, utume alioutekeleza hadi mwaka 2009 alipoteuliwa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita kuwa Balozi wa Vatican nchini Venezuela.

Askofu Marcello Semeraro, Katibu wa Jopo la Makardinali wanane lililoteuliwa na Baba Mtakatifu Francsiko kusaidia kutoa ushauri wa magezi yaliyotolewa na Makardinali anasema kwamba, kati ya mabadiliko yanayotarajiwa ni muundo ambao utaitwa "Sekretarieti ya Papa" kwani jina Katibu mkuu wa Vatican linaweza kuwapotosha watu kwani linaharufu kubwa ya mambo ya kisiasa kuliko hata maisha ya kiroho. Sekretarieti ya Papa inapania kumsaidia Baba Mtakatifu kutekeleza wajibu na dhamana yake kama Askofu wa Roma na Khalifa wa Mtakatifu Petro, kwa kuzingatia uelewa makini wa Kanisa.

Sekretarieti ya Papa itakuwa na wajibu wa kumsaidia Khalifa wa Mtakatifu Petro kutekeleza wajibu na dhamana yake ya uongozi wa Kanisa la Kiulimwengu, kama ilivyofafanuliwa hivi karibuni na Padre Federico Lombardi, Msemaji mkuu wa Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.