Jeshi la Polisi Nchini Tanzania kupitia Kikosi cha Polisi Tazara limefanikiwa kuutokomeza
uhalifu na wizi wa shaba uliokuwa unafanyika katika reli ya Tanzania na Zambia (TAZARA)
baada ya kuishirikisha jamii kwa kutumia dhana ya Polisi jamii na ulinzi shirikishi.
Hayo yalisemwa na Kamanda wa Kikosi cha Polisi TAZARA, Kamishna Msaidizi wa
Polisi (ACP) Rashid Seif wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari wakati
wa Mkutano wa 39 Wakuu wa ulinzi na usalama kutoka mashirika ya reli na bandari kwa
nchi za kusini mwa Afrika (SADC) unaofanyika jijini Dar es Salaam hivi karibuni.
Kamanda
Seif alisema kwa kushirikiana na vikundi vya ulinzi shirikishi vilivyopo katika maeneo
ambayo reli ya Tazara inapita wamekuwa wakipata taarifa ambazo zimesababisha kuzuia
matukio ya wizi wa shaba ambapo tangu mwezi April mpaka sasa hakuna tukio ambalo limetokea
hali ambayo alisema imefanya watumiaji wa reli hiyo kuwa na imani ya kuendelea kusafirisha
mizigo yao.
Aidha alisema Kikosi hicho kwa kushirikiana na uongozi wa Tazara
wameweza kutoa elimu kwa wananchi juu ya utunzaji wa miundominu ya reli ambapo matukio
ya uharibifu wa miundominu yamepungua kwa kiasi kikubwa na lengo ni kuhakikisha uhalifu
unapungua kwa asilimia sabini.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Mkutano huo Bw.
Neil Naidu kutoka Shirika la Reli la Transnet la Afrika kusini alisema malengo ya
mkutano huo ni kubadilishana mbinu za kukabiliana na uhalifu unaovuka mipaka na uhalifu
unaotokea mara kwa mara katika reli na bandari zilizopo katika nchi wanachama SADC.
Alisema
katika kupambana na uhalifu huo ni lazima kufanya kazi kwa pamoja kwa kubadilishana
taarifa za uhalifu na wahalifu pamoja na wananchi kutoa ushirikiano kwa vyombo vya
ulinzi na usalama wa bandari na reli ili kuhakikisha mizigo inayotumia njia hizo za
usafiri inakuwa salama.
Alibainisha kuwa katika mkutano wao huo wa siku tatu
watatoka na maazimio pamoja na mikakati itakayolenga kutokomeza wizi wa mizigo katika
reli, bandari, uharibifu wa miundominu ya reli na makosa yanayovuka mipaka kwa kushirikiana
na wadau wanaosafirisha mizigo kupitia bandari na reli kwa nchi wanachama wa SADC.
Mkutano
huo ulihudhuriwa na wawakilishi kutoka nchi za Botswana, Zambia, Tanzania, Swaziland
na Afrika kusini ambapo mkutano wa mwisho ulifanyika nchini Zambia mwezi Aprili mwaka
huu.