Baba Mtakatifu Francisko mara baada ya kufanya mkutano na Makardinali mapema mwezi
Oktoba na baadaye kukutana na Baraza la Sinodi za Maaskofu, Baba Mtakatifu alionesha
nia yake kwa wajumbe ya kutaka kuwatangaza Makardinali wapya, wakati wa Maadhimisho
ya Siku kuu ya Ukulu wa Mtakatifu Petro, hapo tarehe 22 Februari 2014.
Baba
Mtakatifu pamoja na mambo mengine ameamua kwamba, kutafanyika mkutano wa Makardinali
kutoka sehemu mbali mbali za dunia hapo Mwezi Februari 2014. Hayo yamefafanuliwa kwa
kina na Padre Federico Lombardi Msemaji mkuu wa Vatican.
Anasema kwamba, Baba
Mtakatifu anapenda kuendeleza mapokeo kutoka kwa watangulizi wake kuhusu mikutano
ya Makardinali. Baba Mtakatifu atapata fursa kwanza kabisa kukutana na Kikundi cha
Makardinali wanane aliowateuwa kutoka sehemu mbali mbali za dunia ili kumpatia ushauri
kama ilivyokuwa imependekezwa kwenye mikutano ya Makardinali.
Mkutano huu
unatarajiwa kufanyika hapo tarehe 17 hadi tarehe 18 Februari 2014. Baada ya Mkutano
wa Makardinali, kuanzia tarehe 24 hadi tarehe 25 Februari 2014 kutafanyika Mkutano
wa Baraza la Sinodi. Padre Lombardi anasema, Mwezi Februari, 2014, Baba Mtakatifu
atakuwa na mikutano kadhaa kuhusu maisha na utume wa Kanisa, mikutano inayotarajiwa
kuwahusisha Makardinali wengi zaidi.