2013-10-29 08:47:30

Ujumbe wa Vatican waishukuru Serikali ya Burkina Faso kwa kuunga mkono juhudi za Mfuko wa Yohane II kwa ajili ya Sahel


Kardinali Robert Sarah, Rais wa Baraza la Kipapa linaloratibu misaada ya Kanisa Katoliki Cor Unum na ujumbe wake kutoka Vatican, katika Maadhimisho ya Miaka 30 tangu Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili alipoanzisha Mfuko wa Sahel kama sehemu ya mchakato wa kupambana na Jangwa Barani Afrika, amemtembelea Rais Blaise Compaorè wa Burkina Faso, mjini Ouagadogou.

Lengo la ujumbe wa Vatican kukutana na Rais wa Burkina Faso lilikuwa ni kumshukuru kwa kuendelea kuunga mkono juhudi za Mama Kanisa katika mchakato wa kuwaletea wananchi wanaoishi katika Ukanda wa Sahel maendeleo endelevu.

Serikali ya Burkina Faso imetoa ardhi ambayo itaweza kutumika kwa ajili ya ujenzi wa Makao ya Ubalozi wa Vatican nchini humo. Itakumbukwa kwamba, Makao Makuu ya Mfuko wa Yohane Paulo II yako pia mjini Ouagadogou. Rais wa Burkina Faso anasema ataendelea kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Mfuko wa Yohane Paulo II kwa ajili ya wananchi wa Sahel, kama kielelezo makini cha mapambano dhidi ya baa la njaa, umaskini na mardhi yanayochangiwa kwa kiasi kikubwa na uwepo wa ukame wa kutisha.

Kardinali Sarah anabainisha kwamba, kumekuwepo na mafanikio makubwa yaliyopatika tangu Mfuko wa Yohane Paulo II kwa ajili ya Sahel ulipoanzishwa kunako mwaka 1983 kama njia ya kuonesha mshikamano wa dhati na wananchi wa Ukanda wa Sahel dhidi ya ukame wa kutisha. Bado kuna mengi yanayopaswa kutekelezwa, jambo linalohitaji mshikamano wa dhati na wadau mbali mbali kutoka ndani na nje ya Bara la Afrika.







All the contents on this site are copyrighted ©.