2013-10-29 09:41:34

Marufuku kuhama Ethiopia kwa kisingizio cha kutafuta fursa za ajira!


Serikali ya Ethiopia imepitisha sheria ya muda inayopiga rufuku kwa wananchi wake kuhama kutoka nchini humo kwa ajili ya kutafuta kazi, ili kulinda usalama wa raia wake pamoja na kuzingatia mafao ya nchi na maendeleo ya watu wake.

Wizara ya Mambo ya nchi za nje na ushirikiano wa kimataifa inasema kwamba, wananchi wengi waliokufa maji hivi karibuni kwenye Visiwa vya Lampedusa, Kusini mwa Italia, ni raia wa Ethiopia waliokuwa wanakwenda Ulaya kutafuta fursa za ajira na maboresho ya maisha, lakini kwa bahati mbaya wamefikwa na mauti hata kabla ya kuwasili kwenye nchi husika!

Kutokana na majanga haya yanayoendelea kuongezeka na hivyo kuhatarisha usalama wa maisha ya wananchi wa Ethiopia, Serikali kwa muda imesitisha utoaji wa vibali kwa ajili ya watu wanaotafuta fursa za ajira nje ya nchi. Rufuku hii itaendelea kuwepo hadi pale tatizo hili litakapokuwa limepatiwa ufumbuzi wa kudumu. Ukosefu wa fursa za ajira miongoni mwa vijana nchini Ethiopia ni asilimia 50%, hali inayowasukuma vijana wengi kuikimbia nchi yao hata katika mazingira hatarishi wakiwa na tumaini la kupata walau fursa za ajira Barani Ulaya.

Wahamiaji hawa ambao wamekuwa ni msaada mkubwa katika kukuza na kuimarisha uchumi kwenye nchi za Falme za Kiarabu, Yemen, Afrika ya Kusini, Israel na Ulaya. Kwa bahati mbaya, wahamiaji hawa wanakumbana na mauti hata kabla ya kutimiza ndoto ya kupata fursa za ajira na maisha bora. Taarifa zinaonesha kwamba, baadhi yao wamejikuta wanatumbukizwa kwenye biashara haramu ya binadamu inayoendelea kushamiri kwa kasi sehemu mbali mbali za dunia, jambo linalodhalilisha utu na heshima ya binadamu.







All the contents on this site are copyrighted ©.