2013-10-29 14:43:53

Makardinali na Maaskofu waliofariki dunia 2012- 2013 kukumbukwa kwa Ibada ya Misa Takatifu, tarehe 4 Novemba 2013


Baba Mtakatifu Francisko baada ya kutembelea na kusali kwenye Makaburi ya wananchi wa Roma kama sehemu ya kumbu kumbu ya miaka 20 tangu Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili alipotembelea kwa mara ya kwanza makaburi hayo sanjari na kusali kwa ajili ya kuombea Mapapa waliotangulia mbele ya haki na kuzikwa chini ya Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, Baba Mtakatifu ataadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya Makardinali na Maaskofu, Jumanne, tarehe 4 Novemba 2013.

Ibada ya Misa Takatifu inatarajiwa kuanza hapo saa 5:30 asubuhi kwa saa za Ulaya. Hayo yamebainishwa na Mshereheshaji mkuu wa Ibada za Kipapa Monsinyo Guido Marini siku ya Jumanne, tarehe 29 Oktoba 2013. Mapokeo yanaonesha kwamba, Baba Mtakatifu atawakumbuka na kuwaombea Makardinali na Maaskofu waliofariki dunia katika kipindi cha Mwaka 2012 -2013 kutoka sehemu mbali mbali za dunia.

Mzee mmoja wa busara anabainisha kwamba, "binadamu ana zamu mbili duniani: kuzaliwa ni zamu ya kwanza lakini ni ya bahati nasibu. Zamu ya pili ni mauti; hii ndiyo ya lazima na uhakika". Kila mtu ajiandae kufa kifo chema.

Mtaalam mmoja wa mambo ya Biblia aliwahi kusema, kila mtu hujiandalia watu wa kufika msibani mwake mwenyewe. Ukiwa na watu kwenye misiba yao ukasaidia kuwazika wafu wao, umetoa mwaliko mzuri kwao kwa siku ya msiba wako. Kifupi, ukiwapenda watu wengi na kuwatumikia kwa kujitolea kwao utakuwa umewapa kadi ya mwaliko nzuri ya kufika kwenye mazishi yako. Basi wape kadi ya mazishi yako kwa kushiriki katika mahangaiko ya jirani zako!







All the contents on this site are copyrighted ©.