Utandawazi na teknolojia ya habari visiwaletee "majanga" masomoni!
Mkuu wa mkoa wa Dodoma, Tanzania Dr. Rehema Nchimbi ametoa wito kwa shule zinazomilikiwa
na taasisi za dini kuhakikisha zinaziba mianya yote ya mafundisho yasiyofaa kwa wanafunzi
yanayoletelezwa na mabadiliko ya utandawazi ili ziweze kuzalisha wanafunzi wenye ubora
kielimu na kimaadili.
Dr. Nchimbi amebainisha kuwa hivi sasa kumekuwa na mianya
mingi inayowezesha mafundisho mbalimbali yanayopatikana kupitia maendeleo ya utandawazi
ambayo baadhi yamekuwa na viashiria vinavyochangia kuporomoka kwa tabia, maadili na
mfumo mzima wa wanafunzi kujifunza na kuwaasa wanafunzi kuwa makini sana na masuala
ya utandawazi katika safari zao za masomo kwani, wasipotumia utandawazi ipasavyo itachangia
kuharibikiwa katika masomo yao.
Dr. Nchimbi ameyasema hayo mwishoni mwa wiki
wakati wa mahafali ya tisa ya Sekondari ya Wasichana ya Huruma inayomilikiwa na Shirika
la Watawa Wakatoliki la Misericordia iliyopo Jimbo Katoliki Dodoma ambapo mahafali
hayo yalikwenda sambamba na Jubilei ya miaka 50 tangu watawa hao wa misericodia kuanza
kutoa huduma za elimu nchini Tanzania.
Dr. Nchimbi ameongeza kuwa, katika ulimwengu
wa sasa wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia ya habari na mawasiliano
kumekuwa na matumizi mabaya ya teknolojia hizo yanayofanywa na wanafunzi, matokeo
yake Jamii inazalisha wataalamu na viongozi wasiokuwa na maadili na pia amezitaka
shule ningine nchini Tanzania kujipanga nazo kupambana na tatizo hili.
Mkuu
wa mkoa pia ameshukuru mchango mkubwa unaotolewa na taasisi za dini katika kuhudumia
jamii akiainisha upande wa kutoa huduma za elimu kwa jamii na kusema kuwa Serikali
inatambua na kuthamini sana mchango huo na kuahidi kuendelea kutoa ushirikiano kwa
taasisi hizo za kidini ili kwa pamoja waendelee kuhudumia jamii na kusaidia kuleta
maendeleo ya wengi nchini Tanzania.
Kwa upande wake Askofu mstaafu Mathias
Joseph Isuja wa Jimbo Katoliki Dodoma akitoa historia amesema kuwa miaka ya hapo
awali mfumo wa elimu nchini Tanzania ulikuwa finyu hasa kwa upande wa wasichana kwenda
shule ndipo Kanisa kupitia mashirika yake mbalimbali yakaanza kuwekeza kwenye elimu
ili kumkomboa mwanadamu: kiroho na kimwili
Kwa upande wao wahitimu wa kidato
cha nne wakiwakilishwa na mwanafunzi Ritah George aliyesoma taarifa ya wanafunzi wanaotarajiwa
kuhitimisha masomo yao ya kidato cha nne mwaka hu,u wameomba uongozi wa shule kushughulikia
changamoto za maktaba yenye nafasi za kutosha, vifaa vya kujifunzia kama kompyuta,
viwanja vya michezo na walimu wa michezo.