Rais Kikwete apamba Jubilee ya Miaka 100 ya Ukristo Parokia ya Lugoba, Jimbo Katoliki
Morogoro
Hotuba ya Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
kwenye maadhimisho ya miaka 100 ya kanisa Katoliki, Parokia ya Lugoba, tarehe 27 oktoba,
2013
Mhashamu Baba Askofu, Telesphor Mkude, Askofu wa Jimbo Katoliki la Morogoro; Mhashamu
Baba Askofu Anthony Banzi wa Jimbo Katoliki Tanga; Wahashamu Maaskofu, Viongozi
wa Dini mliopo hapa; Baba Paroko, Padri Constantine Luhimbo; Mapadri, Mashemasi
na Watawa; Ndugu waumini; Wageni waalikwa; Mabibi na Mabwana;
Shukrani
kwa Mwaliko
Niruhusuni niungane na wasemaji walionitangulia kumshukuru
Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema, kwa kutujalia uzima na kutukutanisha hapa katika
Kanisa la Msalaba Mtukuka kusherehekea Jubilei ya miaka mia moja ya Kanisa Katoliki
la Lugoba. Nakushukuru sana Baba Askofu Mkude pamoja na Baba Paroko na waumini wa
Parokia ya Lugoba kwa kunishirikisha katika maadhimisho haya ya kihistoria.
Nawapongeza
sana waumini wa Parokia ya Lugoba kutimiza karne moja tangu ianzishwe. Hayo ni mafanikio
makubwa, hivyo mnastahili kusherehekea kwa nderemo na vinubi. Nawapongeza sana kwa
kuwakumbuka, kuwaenzi na kuwashukuru Padri Cornel na Padri Herman ambao ndiyo waanzilishi
wa Parokia hii miaka 100 iliyopita. Hakika leo ni siku yao wao zaidi pengine kuliko
sisi.
Bila ya juhudi zao, moyo wao wa ujasiri, uvumilivu na kujituma huenda
leo tusingekuwa hapa kufanya maadhimisho haya. Sote tumesikia kuwa mwanzoni mambo
hayakuwa rahisi sana. Lakini, ni ushirikiano wa Wamisionari hao na baadhi ya wenyeji
kama vile Mzee Kinogile, aliyekuwa Mtawala, Mzee Matei, Mzee Lui na wengineo ndiyo
weliowezesha mambo kwenda vizuri na Parokia ikaanzishwa. Nafurahi nao pia mmewatambua
na kuwaenzi.
Kwa ujumla nimefarijika sana kuona kwamba katika kusherehekea
siku ya leo mnawatambua na kuwaenzi watumishi wa Mungu tangu wakati ule mpaka sasa
kwa kazi kubwa waliyoifanya ya kujenga na kuimarisha kanisa kwenye Parokia hii. Kutokana
na kazi yao nzuri waumini wameongezeka, huduma za kiroho zimeimarika na kwamba Kanisa
limetoa mchango muhimu kwa maendeleo ya jamii katika eneo letu hili.
Ndugu
waumini;
Ninyi na mimi ni shuhuda wa jinsi Kanisa Katoliki la Lugoba lilivyochangia
na linavyoendelea kuchangia katika upatikanaji wa huduma za jamii kama vile elimu
na afya bila ya kuwabagua watu kwa imani zao za kumuabudu Mungu. Kwa upande wa afya
tumesikia zahanati zilizojengwa na Kanisa na mipango iliyopo ya kuboresha zaidi huduma
zinazotolewa. Vile vile, tumesikia shule zilizojengwa na kuanzishwa na Kanisa la
Lugoba. Hata mimi ni mmoja wa watu walionufaika kwani nilipata elimu ya darasa la
tano hadi la nane mwaka 1962 mpaka 1965 katika shule iliyokuwa inaitwa St. John Bosco’s
Lugoba Middle School iliyomilikiwa na Kanisa Katoliki Lugoba.
Kunako mwaka
1965, Serikali iliamua kuwa elimu za msingi hazitakuwa na madaraja mawili yaani ya
darasa la kwanza hadi la nne (Primary School) na darasa la tano hadi la nane (Middle
School) badala yake elimu ya msingi ikawa kuanzia darasa la kwanza hadi la saba.
Kufuatia uamuzi huo Lugoba Middle School na Lugoba Primary School ziliunganishwa na
kuwa shule ya Msingi Lugoba. Wakati madarasa tuliyosomea yanaunganishwa na shule
hiyo mpya, iliyokuwa ofisi ya Walimu ikawa zahanati ya Kanisa na yaliyokuwa mabweni
sasa yamekuwa madarasa ya Sekondari ya Lugoba.
Kwa kweli hatuna maneno mazuri
ya kuelezea shukrani zetu kwa Kanisa Katoliki Parokia ya Lugoba kwa mchango muhimu
iliyotoa kwa maendeleo ya watu wa eneo hili, Wilaya ya Bagamoyo na kwingineko nchini.
Watu wengi wamefaidika na wanaendelea kunufaika. Mwenyezi Mungu azidi kuwabariki
ili muendelee kuwahudumia watu katika Parokia yetu ya Lugoba na taifa kwa ujumla.
Tunapenda miaka mia moja ijayo, kwa watakaokuwepo kipindi hicho, wakiri utume huo
usiokifani. Na waseme “hakika wenzetu waliotangulia walikuja kufanya kazi, walikuwa
watu wa kazi”.
Serikali Inathamini Mchango wa Kanisa
Mhashamu
Baba Askofu Mkude; Mabibi na Mabwana;
Napenda kuwahakikishia kuwa
serikali inatambua vyema na kuthamini mambo yote mazuri yanayofanywa na Kanisa Katoliki.
Kabla na hata baada ya uhuru, Kanisa limekuwa mdau muhimu na mshirika muhimu wa Serikali
katika kuhudumia wananchi. Wakati mwingine unakuta huduma za jamii kama zahanati ipo
mahali ambapo hata Serikali bado haijafika. Kutuunga mkono kwa namna hiyo ndiko kumechangia
sana nchi yetu kupiga hatua kubwa kwenye kufikisha huduma kwa jamii nchini.
Ahadi
yangu kwenu ni kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na Kanisa Katoliki pamoja na
madhehebu mengine ya dini kuboresha maisha ya Watanzania. Tutaendelea kupokea ushauri
wenu na kuwashirikisha katika mambo mbalimbali yanayohusu maendeleo ya nchi yetu na
watu wake. Naomba muendelee kushirikiana na Serikali katika kutoa huduma kwa wananchi.
Muendelee kutumia mtandao wenu mpana uliopo nchi nzima kwa ustawi na maendeleo ya
nchi yetu. Lengo letu libaki kuwa moja daima na milele. Tufanye kazi pamoja ili
tufanikiwe zaidi.
Maombi kwa Viongozi wa Dini
Mhashamu Baba
Askofu Mkude, Baba Paroko na viongozi wa dini mliopo;
Naomba muongeze juhudi
za kuhubiri umoja na kutoa mafundisho ya kuhimiza udugu na mshikamano miungoni mwa
Watanzania. Sote tunafahamu kuwa kuna baadhi ya watu wanaofanya juhudi usiku na mchana
kuuvuruga upendo, umoja na mshikamano wa wananchi wa Tanzania. Kwa sasa watu hawa
hawajafanikiwa lakini tuelewe kuwa hawajachoka na wala hawajaaacha. Wana sifa ya
ushetani, maana shetani hachoki wala hakati tamaa katika kuwashawishi wanaadamu kutenda
maovu.
Na, hawa si ajabu wakathubutu tena na tena. Inatupasa na sisi pia
tuwe macho. Naomba msilegeze uzi katika kuwaelimisha waumini wenu waelewe nia mbaya
za watu wasioitakia mema nchi yetu, wawaepuke wala wasiwasikilize. Tudumishe upendo,
umoja na mshikamano wetu. Sisi sote Mungu wetu ni mmoja kwa nini tuchukiane, tubaguane
na hata tuuane kwa sababu ya kutofautiana katika kumuabudu Mungu? Wengine ni ndugu
wa damu kwa nini tufarakane kwa namna ya kumsujudia Muumba wetu? Kila mtu aachwe
kufuata dini anayoipenda na udugu wetu na umoja wetu kama wanadamu ubaki pale pale.
Ipo hatari hata ndugu wa damu tukafarakana kwa sababu ya kuwa dini mbalimbali. Siyo
sawa.
Niliwahi kusema siku za nyuma na leo narudia tena kuwa viongozi wa dini
wanayo nafasi ya pekee katika kufikisha ujumbe huo kwa watu wote. Hii inatokana na
ule ukweli kwamba wanasikilizwa na kuaminiwa sana na waumini wao na watu wengine pia.
Wanasikilizwa na watu wengi. Waumini wakielezwa, wakaelewa na wote wakazingatia kuishi
kama mafundisho ya viongozi wao, nchi yetu itabaki salama. Hakuna mtu atakayefanikiwa
kutufarakanisha na kuichezea amani yetu. Hata kama ni muumini wa dini ya shetani.
Pili,
naomba tuendelee kusaidiana kulea nchi yetu kimaadili. Hakuna siri kwamba kuna mmonyoko
mkubwa wa maadili mema. Vitendo viovu na mambo yasiyoipendeza jamii na yasiyompendeza
Mwenye Mungu yanazidi kuongezeka kwenye jamii. Mambo ambayo siku za nyuma yalikuwa
nadra sana kutokea au kusikika sasa yanakuwa habari za kila siku na wakati mwingine
huonekana ati ndiyo usasa. Matumizi makubwa ya dawa za kulevya, ngono, ubakaji,
watoto kutokuheshimu wakubwa, wazee kutokujiheshimu, ulevi wa kupindukia, vitendo
vya rushwa, uvivu, wizi na idadi kubwa ya ndoa kuvunjika ni vielelezo dhahiri vya
hali mbaya ya kimaadili inayokabili jamii zetu nchini.
Kuporomoka kwa maadili
ni jambo lenye athari mbaya kwa jamii na taifa kwa ujumla. Kunachangia sana kurudisha
nyuma juhudi za kujiletea maendeleo ya nchi yetu na watu wake. Kunaifanya kazi ya
kuondoa umaskini kuwa ngumu na kuongeza watoto wa mitaani. Kunachangia kuenea kwa
maambukizi ya UKIMWI. Kunaongeza uhalifu wa aina mbalimbali nchini pamoja na mauaji.
Mimi naamini kwa dhati kuwa watu wakishika mafundisho ya dini, wakamuogopa Mwenyezi
Mungu, maovu mengi yatapungua. Hayawezi kuisha kabisa lakini yatapungua sana. Ndiyo
maana narejea ombi langu ninalolitoa mara kwa mara kwa viongozi wa dini zote. Tusaidiane
kulea taifa letu kimaadili. Tuweke mkazo zaidi kwa vijana kwa sababu, kwanza wao ndio
walengwa wakuu wa maovu yanayotendeka. Lakini pili, wao ndio taifa la leo na kesho,
ndio warithi wa taifa letu. Tukiwaandaa vyema, mustakabali wa taifa letu na watu wake
utakuwa kwenye mikono salama. Tukishindwa leo, tutalia na kusaga meno kesho. Taifa
letu litakuwa mashakani.
Mwisho
Kwa kumalizia nawapongeza wote
walioshiriki kwa namna moja ama nyingine kuandaa sherehe hizi. Kwa kweli zimefana
sana na watu wote hapa ni mashahidi. Nakushukuru kwa mara nyingine tena Mhashamu Baba
Askofu na Baba Paroko kwa uongozi wenu uliotukuka. Nimefurahi sana kujumuika nanyi
katika maadhimisho haya. Naomba tuendelee kushirikiana kuleta maendeleo zaidi kwenye
Parokia yetu na nchi yetu kwa ujumla. Tukiunganisha nguvu zetu, daima ushindi utapatikana.
Naomba tuamue kuwa washindi. Tumsifu Yesu Kristo.