2013-10-28 07:50:48

Marehemu Askofu Mwanyika: alikuwa mcheshi, mchapakazi, mbunifu, mtu wa watu na kiongozi aliyethubu!


Askofu mstaafu Raymond Mwanyika wa Jimbo Katoliki Njombe, aliyefariki dunia hapo tarehe 24 Oktoba 2013 anatarajiwa kuzikwa siku ya Jumanne tarehe 29 Oktoba 2013. RealAudioMP3

Askofu mkuu Josephat Lebulu wa Jimbo kuu la Arusha, Tanzania kwa njia ya Radio Vatican anapenda kutuma salam zake za rambi rambi kwa Askofu Alfred Maluma wa Jimbo Katoliki Njombe pamoja na Familia ya Mungu Jimboni humo. Anasema, amezipokea habari za msiba wa Askofu mstaafu Mwanyika kwa majonzi, masikitiko na matumaini. Anaungana na Familia yote ya Mungu nchini Tanzania kwa ajili ya kumwombea Marehemu Askofu Mwanyika ili aweze kupata furaha ya uzima wa milele.

Anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuuga mfano wa huduma na majitoleo yaliyooneshwa na Marehemu Askofu Mwanyika enzi ya uhai wake. Alikuwa ni mcheshi, mchapakazi na mbunifu. Alikuwa ni kiongozi mpenda maendeleo, aliyebuni na kupanga mikakati ya maendeleo inayogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili. Marehemu Askofu Mwanyika, alitoa kipaumbele cha kwanza kwa huduma za kichungaji Jimboni mwake. Kwa hakika ni kiongozi aliyethubutu kutenda na kamwe hakukata tamaa kutokana na magumu au vizingiti alivyokumbana navyo.

Askofu mkuu Lebulu anasema, Marehemu Askofu Mwanyika alikuwa ni mtu wa watu kwa ajili ya watu; alishiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania. Alitegemewa sana kwa ushauri wake makini na wenye busara. Askofu mkuu Lebulu anamshindikiza Marehemu Askofu Mwanyika na Maaskofu wengine waliomtangulia katika huduma ya Kiaskofu kwa sala na sadaka ya Misa Takatifu.







All the contents on this site are copyrighted ©.