2013-10-28 10:11:12

Kuna idadi kubwa ya wanawake magerezani, wanaonyanyaswa na kudhulumiwa kijinsia!


Taarifa ya Umoja wa Mataifa kuhusu makosa dhidi ya wanawake iliyotolewa hivi karibuni inaonesha kwamba, kuna idadi kubwa ya wanawake ambao wako magerezani, wanadhulumiwa kijinsia na kuishi katika mazingira hatarishi zaidi, ikilinganishwa na wafungwa wa kiume. Hayo yamebainishwa na Bi Rashida Manjoo, mtaalam wa masuala ya wanawake, alipokuwa anazungumza hivi karibuni kwenye Baraza kuu la Umoja wa Mataifa.

Vitendo vya jinai, mmong'onyoko wa kimaadili, biashara haramu ya dawa za kulevya na ujambazi ni kati ya makosa ambayo wanawake wengi wanashutumiwa kuyafanya na hivyo kujikuta wakiwa wamefungwa pingu magerezani. Takwimu zinaonesha kwamba, katika kipindi cha miaka ya hivi karibuni kumekuwepo na ongezeko kubwa la idadi ya wanawake wanaojihusisha na biashara haramu ya dawa za kulevya na kwamba, wengi wao wamekamatwa na kufikishwa kwenye mkondo wa sheria na kwa sasa wanatumikia adhabu zao.

Taarifa za hali ya wanawake magerezani zinaonesha kwamba, wanawake wanakabiliwa na hali tete ya maisha, hii ikiwa ni nyanyaso na dhuluma za kijinsia wanapokuwa magerezani; wakati mwingine wanalazimishwa kujihusisha na biashara haramu ya ngono. Kuna kundi kubwa la watoto wanaoishi mama zao magerezani, hali ambayo inahatarisha malezi na makuzi ya watoto hawa.

Mtetezi wa haki msingi za binadamu kutoka Umoja wa Mataifa anasema kwamba, kuna haja kwa Serikali kufanya upembuzi wa kina zaidi ili kubaini sababu zinazopelekea wanawake wengi kutupwa magerezani. Serikali zinawajibu wa kulinda na kuwatetea raia wake dhidi ya nyanyaso na dhuluma za kijinsia.







All the contents on this site are copyrighted ©.