Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete amemtumia Salamu
za Rambirambi Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mheshimiwa Bernard
Membe kufuatia kifo cha Mwanadiplomasia na Mwanasiasa Mkongwe, Balozi Isack Sepetu
aliyefariki dunia tarehe 27 Oktoba, 2013 katika Hospitali ya TMJ ya Jijini Dar es
Salaam alikopelekwa kwa matibabu ya ugonjwa wa Kisukari na Kiharusi.
Marehemu
Balozi Isack Sepetu, enzi za uhai wake, aliwahi kushika nyadhifa mbalimbali za juu
Serikalini kuanzia miaka ya Sabini ambapo aliwahi kuteuliwa kuwa Naibu Waziri wa
Mambo ya Nchi za Nje katika Serikali ya Awamu ya Kwanza, Waziri wa Habari, Utangazaji
na Utalii katika Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.
Katika miaka ya Tisini, aliteuliwa
kuwa Waziri wa Nchi, Mipango na Uchumi katika Serikali ya Mapinduzi Zanzibar iliyoongozwa
na Dr. Salmin Amour. Akiwa Balozi wa Tanzania, Marehemu aliiwakilisha nchi katika
Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC) na uliokuwa Muungano wa Nchi za Kisovieti za
Kisoshalisti za Urusi (USSR) ambayo kwa sasa ni Russia.
“Nimepokea kwa mshtuko
na masikitiko makubwa taarifa za kifo cha Mwanasiasa na Mwanadiplomasia Mashuhuri,
Balozi Mstaafu, Mheshimiwa Isack Sepetu aliyefariki dunia katika Hospitali ya TMJ
Jijini Dar es Salaam alikopelekwa kwa matibabu ya ugonjwa wa Kisukari na Kiharusi
tarehe 27 Oktoba, 2013”, amesema Rais Kikwete katika Salamu zake za Rambirambi.
Rais
Kikwete amesema alimfahamu Marehemu Balozi Isack Sepetu, enzi za uhai wake, kama Mwanasiasa
na Kiongozi mwenye bidii na uwezo mkubwa wa uongozi ambaye alidhihirisha uaminifu
na uadilifu wake katika nyadhifa mbalimbali alizowahi kushikilia katika Awamu zote
za Uongozi Tanzania Bara na Zanzibar. Balozi Sepetu aliwahi pia kuwa Mjumbe wa Halmashauri
Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwa nafasi ya kuteuliwa na Mwenyekiti wa Chama, na
kukitumikia Chama kwa uaminifu na uadilifu mkubwa.
“Natambua hata baada ya
kustaafu, Marehemu Balozi Isack Sepetu aliendelea kuaminiwa katika utumishi wake,
na hivyo kuteuliwa kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Vitega Uchumi
Zanzibar (ZIPA) katika Serikali ya Mapinduzi Zanzibar inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt.
Ali Mohamed Shein, na pia Mjumbe wa Bunge la Afrika Mashariki hadi mauti yalipomkuta”,
amesema Rais Kikwete, na kuongeza,
“Kutokana na msiba huo mkubwa, ninakutumia
wewe Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mheshimiwa Bernard Membe
Salamu zangu za Rambirambi kwa kumpoteza Mwanadiplomasia na mmoja wa Viongozi shupavu
katika nchi yetu, Marehemu Balozi Isack Sepetu”.
“Kupitia kwako, naomba pia
Salamu zangu za Rambirambi na pole nyingi ziwafikie Wanafamilia ya Marehemu kwa kumpoteza
Kiongozi na Mhimili Madhubuti wa Familia. Nawaomba wote wawe na moyo wa uvumilivu
na subira katika kipindi hiki kigumu cha maombolezo kwani yote ni mapenzi yake Mola”.
Rais
Kikwete amewahakikishia Wanafamilia ya Marehemu Balozi Isack Sepetu kuwa yuko pamoja
nao katika kipindi chote cha majonzi kufuatia kifo cha mpendwa wao. Namwomba Mwenyezi
Mungu, Mwingi wa Rehema aipokee na kuilaza Mahala Pema Peponi Roho ya Marehemu Balozi
Isack Sepetu, Amina.