2013-10-27 14:13:26

Familia zawasha moto wa imani kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, kukutana tena Septemba 2016!


Askofu mkuu Vincenzo Paglia, Rais wa Baraza la Kipapa la Familia anasema, Maadhimisho ya Mwaka wa Imani kwa Familia yameziwezesha familia kutoka sehemu mbali mbali za dunia kufanya hija ya maisha ya kiroho, wametambua na kuona uwepo endelevu wa Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu katika hija ya maisha yao kama ilivyokuwa kwa wafuasi wa Emmaus.

Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu yanaendelea kuwaunganisha wanafamilia, ili waweze kujisikia kuwa ni mwili mmoja na roho moja. Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro kwa muda wa siku mbili umegeuka kuwa ni Emmaus ya Familia duniani, kiasi cha kusikia uwepo endelevu wa Kristo kati yao!

Familia zinapenda kumkaribisha Kristo kati yao ili awaangazie mwanga katika safari ya maisha yao, awasaidie nyakati za shida na magumu; awalinde dhidi ya mawimbi mazito ya bahari; akae pamoja na wadogo ili wazidi kukua kimo na hekima; vijana wadumu katika matumaini na kamwe wasiruhusu watu wawapokonye tumaini hilo; wazazi wawe na ukarimu pamoja na upendo wa dhati; wazee waonje fukuto la jirani zao.

Askofu mkuu Paglia amemhakikishia Baba Mtakatifu kwamba, Maadhimisho ya Mwaka wa Imani kwa familia, kimekuwa ni kipindi cha sala, shangwe na tafakari ya Neno la Mungu na kwamba, wameonja uwepo wake wa kibaba na kimama kati yao! Kwa mara ya kwanza katika maisha na utume wake, Baba Mtakatifu Francisko amekutana na kuzungumza na Familia.

Ni matumaini ya Askofu mkuu Paglia kwamba, wataweza kuunganika pamoja hapo Septemba 2016 kwa ajili ya Maadhimisho ya Siku ya Familia Kimataifa. Familia zinaporudi katika maisha ya kawaida, zinaendelea kuhamasishwa kutolea ushuhuda wa imani kwa njia ya mshikamano wa upendo kwa kutambua umuhimu wa familia duniani. Moto wa familia uliowashwa kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, utaendelea kuenea sehemu mbali mbali za dunia.







All the contents on this site are copyrighted ©.