2013-10-27 09:34:30

Familia ni urithi mkubwa wa binadamu na salama ya wanyonge!


Askofu mkuu Vincenzo Paglia, Rais wa Baraza la Kipapa la Familia akimkaribisha Baba Mtakatifu Francisko kushiriki katika mkesha wa Maadhimisho ya Mwaka wa Imani kwa ajili ya familia, Jumamosi, tarehe 26 Oktoba 2013. Alimwonesha Baba Mtakatifu jinsi ambavyo familia za Kikristo zilivokuwa zinafurahia imani yao kwa Kristo na Kanisa lake.

Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro ulikuwa umesheheni wajumbe wa familia kutoka katika nchi zaidi ya 75. Walikuwa wamekusanayika ili kuombea amani, upendo na utulivu, dhidi ya vita, njaa na magonjwa yanayoendelea kutishia usalama wa maisha na ustawi wa familia sehemu mbali mbali za dunia. Familia za Kikristo zilikuwa zimekusanyika kusherehekea zawadi ya imani inayosambaratisha milima ya ubinafsi na upweke hasi na hivyo kuwafanya kuwa ni sehemu ya Familia kubwa ya waamini ambalo ni Kanisa.

Askofu mkuu Paglia anasema, hata katika familia za Kikristo kuna shida na mahangaiko yake, lakini hawawezi kukata tamaa, kwa kutambua umuhimu wa familia kama kito cha thamani duniani. Ndani ya familia humo kuna bubujika upendo unaowawezesha kuvuka vikwazo vya ubinafsi na kuwaendea jirani zao, ili kujenga na kuimaarisha mshikamano wa upendo unaoikumbatia dunia nzima, ili familia ziweze kuwa na umoja.

Familia za Kikristo zilizokuwa zimekusanyika kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro anasema Askofu mkuu Paglia ni kielelezo cha mshikamano na familia zote zinazoteseka nchini Syria kutokana na vita, ili ziweze kuonja upendo na mshikamano kutoka kwa Mama Kanisa. Familia ndio urithi mkubwa kwa binadamu wote; ni mahali pa amani kwa wanyonge.

Familia ndicho kiini cha uwepo wa waamini wengi kutoka sehemu mbali mbali za dunia kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, ili kwa pamoja waweze kujenga na kuimarisha Familia ya Watu wa Mungu, yaani Kanisa.







All the contents on this site are copyrighted ©.