2013-10-26 08:13:56

Kanisa kwa kuridhia itifaki ya ushirikiano na Serikali halitafuti upendeleo wa pekee, bali kushiriki katika mchakato wa maendeleo endelevu!


Vatican na Serikali ya Equatorio Guinea, tarehe 25 Oktoba 2013 zimebadilishana hati za maridhiano ya itifaki ya ushirikiano baina ya Serikali hizi mbili, tukio ambalo limehudhuriwa na viongozi wa serikali na Kanisa. Ujumbe wa Serikali umeongozwa na Rais Teodoro Obiang nguema Mbasogo na Askofu mkuu Dominic Mamberti ameongoza ujumbe kutoka vatican katika hafla hii fupi iliyofanyika mjini Vatican.

Itakumbukwa kwamba, kunako tarehe 13 Oktoba 2012, Vatican na Serikali ya Equatorio Guinea zilitiliana sahihi mkataba wa ushirikiano kati ya Serikali na Kanisa, mkataba ambao kwa sasa umeridhiwa na pande zote mbili.

Itifaki ya Mkataba kati ya Serikali na Kanisa unalitambua Kanisa kisheria na kwamba, Kanisa liko huru kutekeleza wajibu na dhamana yake ndani ya jamii, kwa kushirikiana na Serikali kwa ajili ya mafao na maendeleo endelevu ya wananchi wa Equatorio Guinea.

Askofu mkuu Dominic Mamberti, Katibu mkuu wa Mambo ya nchi za nje na ushirikiano wa kimataifa mjini Vatican kwa niaba ya Askofu mkuu Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican, amewashukuru wadau wote waliowezesha hatimaye, itifaki ya ushirikiano kati ya Vatican na Serikali ya Equatorio Guinea kuweza kufikiwa baina ya pande hizi mbili. Haya ni matunda ya majadiliano ya kina kati ya Serikali na Kanisa kwa kutambua na kuthamini mchango wa Kanisa katika mchakato wa maendeleo endelevu kwa wananchi wa Equatorio Guinea

Hii ni huduma inayopania maendeleo ya mtu mzima: kiroho na kimwili lakini zaidi katika sekta ya elimu na afya. Kwa maridhiano haya, Kanisa litaweza kutekeleza dhamana na utume wake kwa ajili ya mafao ya wengi. Kanisa halitafuti upendeleo wala faida yake binafsi, bali linapenda kuchangia katika mchakato wa maendeleo endelevu yanayogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili, likisukumwa na kipaji cha ugunduzi na huru kutekeleza wajibu huu msingi unaopania pamoja na mambo mengine, ujenzi wa Jamii inayosimikwa katika misingi ya haki na amani.

Askofu mkuu Mamberti anasema, Kanisa litaweza kutekeleza kwa kina zaidi dhamana hii ikiwa kama misingi iliyobainishwa na itifaki hii itazingatiwa na kufanyiwa kazi na pande zote mbili.










All the contents on this site are copyrighted ©.