2013-10-25 09:20:59

Utume wa Familia kwa familia za kijeshi nchini Marekani!


Askofu mkuu Timothy Broglio wa Jimbo kuu la Kijeshi Marekani katika mahojiano maalum na Radio Vatican anabainisha kwamba, utume wa familia ni kati ya mambo makuu yanayopewa kipaumbele cha pekee na Jimbo lake la kijeshi linalowahudumia wanajeshi pamija na familia zao.

Familia ni kati ya taasisi ambazo zimeathirika sana kutokana na migogoro ya kivita na kijamii inayowahusisha wanajeshi kutoka Marekani, kwani kutokana na kazi yao, hulazimika kuziacha familia kwa kipindi kirefu hali ambayo ni hatari kwa ustawi na maendeleo ya familia husika. Kwa vile vita haina macho, baadhi yao hupoteza maisha, hupata vilema vya kudumu na wakati mwingine kuchanganyikiwa. Athari zote hizi kwa kiasi kikubwa zinabebwa na familia husika.

Anasema, kutokana na athari za myumbo wa uchumi kimataifa, Kanisa limeendelea kuwa mstari wa mbele kusaidia kwa hali na mali familia zinazojikuta ziliogelea katika umaskini wa hali na kipato. Sera ya kujali maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii ni kati ya mikakati ya Kanisa Katoliki nchini Marekani.

Huu ni mwelekeo pia unaooneshwa na Serikali ya Marekani kwa Rais Barack Obama kumteuwa Bwana Kenneth Hackett kuwa Balozi Mpya wa Marekani mjini Vatican. Huyu ni kiongozi ambaye kwa miaka mingi amejihusisha na masuala ya huduma kwa maskini na watu wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii, kuteuliwa kwake kuwa Balozi ni changamoto kwa Marekani kuonesha kwamba, inajali na kuguswa na mahangaiko ya watu sehemu mbali mbali za dunia.

Askofu mkuu Timoth Broglio anasema, Maadhimisho ya Siku ya Familia Duniani kwa Mwaka 2016 yatafanyika Jimbo kuu la Philadelphia, Marekani. Ni matumaini yake kwamba, Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani litajitahidi kuhakikisha kwamba, maadhimisho haya yanafanikiwa kama ilivyopangwa. Mara ya mwisho Maadhimisho haya yalipofanyika Jimbo kuu la Milano, Kaskazini mwa Italia zaidi ya waamini millioni moja walihudhuria wakati wa kufunga rasmi Maadhimisho hayo kwa Ibada ya Misa Takatifu iliyoongozwa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa XVI.







All the contents on this site are copyrighted ©.