TRA ni "janga" la ufanisi Bandari ya Dar es Salaam
Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe ameishutumu Mamlaka ya Mapato (TRA) kuwa
ni kikwazo kwake katika utekelezaji wa mipango mbalimbali ya kuboresha bandari ya
Dar es Salaam ikiwa ni pamoja na utekelezaji wa mpango wa matokeo makubwa sasa (BRN).
Dk.
Mwakyembe alisema watu wengi wanaoitumia bandari ya Dar es Salaam (TPA) wanalalamikia
madudu wanayofanya TRA hasa tatizo la kufeli kwa mfumo wa mawasiliano ya kompyuta
unaotumiwa na mamlaka hiyo kutoza kodi mbalimbali.
Alitoa shutuma hizo baada
ya kutakiwa na Waziri Mkuu Mizengo Pinda ajibu baadhi ya maswali yaliyoulizwa na Watanzania
wanaofanya biashara na wale wanaoishi katika jiji la Guangzhou, jimbo la Guangdong
ambalo ni jiji kubwa la biashara lililoko kusini mwa China. Alhamisi, Oktoba 24, 2013
Waziri Mkuu alihitimisha ziara yake ya China kwa kufanya mazungumzo na Watanzania
wanaoishi katika jimbo hilo maarufu kwa biashara.
Bw. Stanley Mwakipesile
ambaye ni mfanyabiashara wa Kariakoo anayefuata bidhaa zake katika jimbo la Guangzhou,
katika hoja zake alisema utoaji wa mizigo katika bandari ya Dar es Salaam ni tatizo
kubwa kutokana na mfumo wa kutoza kodi unaotumiwa na TRA kutofanya kazi siku zingine
na hivyo kusababisha mteja kutozwa fedha nyingi.
Mfanyabiasahra huyo alisema
kutokana na kero hiyo, wafanyabiashara wengi kutoka nchi jirani wameikimbia bandari
hiyo na sasa wanatumia bandari ya Mombasa jambo ambalo alisema ni hasara kwa nchi.
“Inakuwaje kila siku pale TRA system inakuwa down? Kuna urasimu mwingi tu pale lakini
cha ajabu wakati wao ndio hawafanyi kazi, lakini mteja anatozwa eti kachelewesha kutoa
mzigo,” alisema Mwakipesile.
Dk. Mwakyembe katika kujibu hoja za mfanyabiashara
huyo alikiri kuwepo kwa tatizo hilo na akasema eneo linalolalamikiwa sana ni TRA ni
kuwatoza wateja tozo za ziada hata kipindi ambacho watendaji wa mamlaka hiyo hawafanyi
kazi kwa kisingizio cha mfumo kutofanya kazi (system down).
“Mheshimiwa Waziri
Mkuu kwa kweli TRA ni tatizo, hasa hili la system down kwa kweli ni kero na linawaumiza
watu wengi wanaotumia bandari yetu. Ni lazima tukae tuone namna ya kutatua tatizo
hili,” alisema Mwakyembe.
Alisema licha ya kuwepo agizo kutoka serikalini la
kutaka TPA na TRA wafanye kazi saa 24, lakini watendaji wa TRA wanafanya kazi kwa
saa 12 tu na wanalala kwa siku 10 katika mwezi mzima.
Alisema wakati TRA wanaenda
kulala, mteja hahudumiwi na wanapokuja kuendelea na kazi kesho yake, wanawatoza
wateja tozo ya kuchelewesha mzigo wakati makosa siyo ya wateja bali ni ya watendaji
wa mamlaka hiyo ya kukusanya kodi kwa Tanzania. “Sisi TPA hatulali; lakini wenzetu
hawa wanalala, inakuwaje wanaenda kulala wakati mizigo imerundikana pale bandarini?
Kwa kweli hawa watu ni lazima tushughulike nao.
“Mimi nimesaini BRN, Rais anataka
kuona mwaka 2015 shehena inaongezeka pale, na kufikia tani 18 sasa yule atakayekaa
mbele yangu kunikwamisha mie nitampitia,” alisema Dk Mwakyembe na kushangiliwa kwa
nguvu na watanzania hao. Hata hivyo aliwatoa hofu Watanzania kwa bandari ya Dar es
Salaam inafanya kazi vizuri na kila mwaka shehena imekuwa inaongezeka, hali inayoonyesha
kuwa batu nchi nyingi ikiwemo Zimbabwe bado zinatumia bandari hiyo.