2013-10-25 07:45:37

Familia inapaswa kulindwa, kutetewa na kuhifadhiwa kwa haki na nguvu zote!


Katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani kwa ajili ya Familia, Askofu Telesphor Mkude wa Jimbo Katoliki Morogoro, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Tume ya Familia, Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania anakiri kwamba, familia ni tunu ya pekee katika maisha ya mwanadamu ambaye ameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu, hali inayoonesha ule utukufu wa Mungu katika maisha ya mwanadamu. RealAudioMP3

Utukufu huu umechafuliwa kutokana na uwepo wa dhambi ya asili pamoja na mapungufu yanayoendelea kujitokeza katika maisha ya mwanadamu.

Mwanaume na mwanamke wameumbwa na Mungu ili waweze kukamilishana, kusaidiana na kutakatifuzana katika hija ya maisha yao hapa duniani. Kilele cha kazi ya uumbaji ni mwanadamu anayeshiriki dhamana na wajibu wa kuendeleza kazi ya uumbaji iliyoanzishwa na Mwenyezi Mungu mwenyewe. Kutokana na wajibu huu, zawadi ya uhai inapaswa kulindwa na kutetewa tangu pale mimba inapotungwa.

Ikumbukwe kwamba, mtoto ni zawadi kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu, hata familia zile ambazo hazijabahatika kupata watoto, wao kimsingi wanaunda familia. Askofu Mkude anasema, hakuna mtoto anayezaliwa kwa bahati mbaya. Sera na mikakati inayolenga kudhibiti na kukumbatia utamaduni wa kifo inakwenda kinyume kabisa cha mpango wa Mungu katika maisha ya mwanadamu. Hiki ni kielelezo cha ubinafsi wa hali ya juu kuliko maendeleo, tija na ustawi wa mwanadamu.

Familia inapaswa kupewa kipaumbele cha kwanza katika mikakati, mipango na sera za Serikali na wadau mbali mbali. Familia ipewe heshima na haki zake msingi; itambuliwe na kuthaminiwa. Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto katika mahubiri yake kwenye Siku ya Familia Kimataifa iliyofanyika Jimbo kuu la Milano, Kaskazini mwa Italia na kuhudhuriwa na bahari ya wanafamilia kutoka sehemu mbali mbali za dunia alisema kwamba, familia inapaswa kukuza na kudumisha umoja, upendo na mshikamano wa dhati.

Serikali na watunga sera wajitahidi kuenzi tunu msingi za maisha ya kifamilia; familia ipewe haki ya kuishi kwa pamoja; iwe na uhuru wa malezi na elimu kwa watoto wake. Kwa maneno mengine familia inapaswa kulindwa, kutetewa na kuhifadhiwa kwa haki na nguvu zote. Askofu Mkude anasema, familia inapaswa kupewa fursa ya kufanya kazi ili iweze kutekeleza dhamana na wajibu wake.







All the contents on this site are copyrighted ©.