2013-10-25 11:43:49

Epukeni kuwa ni watumwa wa dhambi! Msipindishe majina ya dhambi kukwepa ukweli!


Wakristo wanapaswa kujenga ujasiri, ukweli na uwazi wa kuungama dhambi zao bila kuogopa wala kuficha jambo lolote kama njia ya kuonja tena huruma na upendo kutoka kwa Yesu Kristo na kwa njia hii waamini wanaweza kugundua tena huruma ya Mungu katika maisha yao.

Kuna baadhi ya waamini wanapata shida sana kwenda kuungama dhambi zao mbele ya Padre, hali ambayo inadhohofisha umuhimu wa Sakramenti ya Upatanisho miongoni mwa waamini.Mtakatifu Paulo anapowaandikia Warumi anasema kwamba, dhambi iliyoko ndani mwake ndiyo inayompelekea kutenda kinyume cha utashi wake. Haya ni mambo yanayojitokeza katika maisha ya imani, kwani ubaya bado unamwandama mwanadamu.

Hayo yamesemwa na Baba Mtakatifu Francisko wakati wa mahubiri yake kwenye Kikanisa cha Mtakatifu Martha kilichoko mjini Vatican, Ijumaa tarehe 25 Oktoba 2013. Anawahimiza waamini kupambana kufa na kupona dhidi ya dhambi, ili kuonja huruma na upendo wa Mungu katika maisha yao. Waamini wajifunze kuepuka kuwa ni watumwa wa dhambi kwa kumpatia Yesu nafasi katika mioyo na maisha yao; wawe na ujasiri wa kuiita dhambi kwa jina kamili na wala si kwa kuipachika majina ya bandia, kwani hiki ni kielelezo cha unyenyekevu mbele ya Mwenyezi Mungu.

Waamini wanachangamotishwa na Mama Kanisa kuungama dhambi zao, ili kumpatia Mwenyezi Mungu utukufu kwani Yeye ndiye anayemkomboa mwanadamu kutoka katika lindi la dhambi na mauti. Baba Mtakatifu anasema, mwamini hawezi kuungama dhambi zake kwa njia ya mitandao ya jamii, bali ni kumwendea Kristo kwa kutambua kwamba, yeye ni mdhambi mbele ya Padre ambaye ni Wakili wa Kristo.

Waamini wawe na unyenyekevu wa kuona ubaya wa dhambi ili waweze kutubu na kuungama mbele ya Mwenyezi Mungu. Wawe wakweli, wa wazi na wanyenyekevu kama watoto wadogo. Kumwonea Mungu aibu ni kielelezo cha neema, kama alivyofanya Mtakatifu Petro, alipokutana na Yesu, akajiona mtupu mbele ya utakatifu na ukuu wa Kristo.







All the contents on this site are copyrighted ©.