Kardinali Mauro Piacenza, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya Makleri hivi
karibuni amezungumzia kuhusu: toba na wongofu wa Makleri katika Maadhimisho ya Mwaka
wa Imani, akichambua kwa namna ya pekee umuhimu wa Makleri kufanya toba kama msingi
thabiti unaowawezesha Makleri kuwaimarisha ndugu zao katika imani. Kardinali Piacenza
alikuwa anazungumza na Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania, kama sehemu ya Maadhimisho
ya Mwaka wa Imani.
Daraja takatifu
la Upadre linawawezesha mapadre kupokea chapa ya Roho Mtakatifu inayowawezesha kujitoa
bila ya kujibakiza kwa ajili ya kutangaza Habari Njema ya Wokovu hadi miisho ya dunia.
Hapa ni mahali ambapo, imani inapyaishwa tena kadiri Padre anavyojiweka mbele ya Mwenyezi
Mungu, kwa toba na wongofu wa ndani, jambo ambalo linamwezesha kuzaa matunda ya ajabu
katika maisha na utume wa Kanisa.
Yote haya yanawezekana ikiwa kama Padre
ana imani madhubuti na anatambua kile anachopaswa kutenda na anakitenda kwa ari na
moyo mkuu. Mapadre watambue kwamba, wao kimsingi ni watu wa imani, waliopewa dhamana
ya kuwaimarisha ndugu zao katika Kristo ndani ya Kanisa kwa kujitoa bila ya kujibakiza
kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake.
Jambo hili ni muhimu sana katika ulimwengu
wa utandawazi ambamo ubinafsi unaonekana kushika kasi ya ajabu, Mapadre wasipokuwa
makini wanaweza kujikuta wakitumbukia katika ubinafsi kutokana na ubinadamu wao na
hivyo kushindwa kutekeleza wajibu na dhamana waliyokabidhiwa na Mama Kanisa walipopewa
Daraja Takatifu la Upadre.
Kardinali Piacenza anasema, Mapadre wanayo dhamana
ya kuwahudumia Watu wa Mungu kiroho na kimwili: kwa njia ya huduma mbali mbali za
kijamii sanjari na Uinjilishaji, kwani kwa njia ya Fumbo la Umwilisho; Neno wa Mungu
amejifanya mtu, katika mambo yote alikuwa sawa na binadamu isipokuwa hakutenda dhambi.
Toba na wongofu kwa Mapadre wakati huu wa Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, ni changamoto
kwa Makleri kusimama kidete katika imani, huku wakiwa na ari mpya katika maisha yao
ya kiroho yanayowasukuma kuwaimarisha ndugu zao katika Kristo, kama dhamana waliyokabidhiwa
na Mama Kanisa.
Wahakikishe kwamba, wanatumia nyenzo mbali mbali zilizoko
mbele katika kutekeleza wajibu huu msingi katika maisha na utume wa Kanisa. Makleri
ni vyombo vya Roho Mtakatifu katika kuwatakatifuza Watu wa Mungu, ndiyo maana kuna
uhusiano wa karibu kabisa kati ya toba, wongofu wa ndani, karama za Roho Mtakatifu
na utume wanaopaswa kuutekeleza kwa niaba ya Mama Kanisa.
Kardinali Mauro Piacenza
anawaalika Mapadre kutolea ushuhuda wa imani yao kwa Kristo na Kanisa lake, huku wakiendelea
kuijenga na kuiimarisha kwa njia ya Sakramenti za Kanisa, Tafakari ya Neno la Mungu,
Matendo ya toba na huruma. Huduma kwa Familia ya Mungu, ipewe kipaumbele cha kwanza
katika maisha na utume wa Mapadre, wakitambua kwamba, hata wao, Mwenyezi Mungu anawasubiri
kuona wakifanya hija ya toba na wongofu wa ndani kwa unyenyekevu na moyo mkuu.
Kama
binadamu wana utajiri mkubwa lakini pia wanayo mapungufu yao yanayoweza kuwa ni kikwazo
katika maisha na utume wao ndani ya Kanisa, kumbe, toba na wongofu wa ndani ni jambo
la msingi, linalowawezesha kuwa karibu zaidi na Mwenyezi Mungu, tayari kuwaimarisha
ndugu zao katika imani.
Mapadre wakumbuke kwamba, utume wao ni mtakatifu,
lakini umewekwa kwenye chombo cha udongo kinachohitaji uangalifu mkubwa, ili kutekeleza
na kuadhimisha Mafumbo ya Kanisa kwa unyenyekevu, huku wakitafakari kazi ya Mungu
inayowaalika, inayowapatia nafasi ya kufanya toba na kuchuchumilia wongofu wa ndani;
kwani neema ya Mungu inaponya na kutakatifuza.
Ni mwaliko wa kumtangaza Mwenyezi
Mungu ambaye wamemtafakari, wakamwona na kumwadhimisha; huyu ndiye Neno wa Mungu aliyejifanya
mtu! Kwa kutambua ukuu wa Yesu Kristo kama Mkombozi wa dunia; aliyeteswa, akafa na
kufufuka kutoka katika wafu; Kuhani mkuu wa Agano Jipya na la Milele; Mwaka wa Imani
unakuwa ni hazina kubwa kwa Mapadre kutubu na kumwongokea Mwenyezi Mungu, ambaye ni
mwingi wa huruma na mapendo.
Kardinali Mauro Piacenza anaendelea kufafanua
kwamba, utekelezaji wa majukumu ya maisha na wito wa Kipadre kwa uaminifu, unyenyekevu
na moyo mkuu ni jambo ambalo linaleta furaha kwa Mapadre ili kuwaimarisha ndugu zao
katika Kristo. Toba na wongofu wa ndani kwa Mapadre ni chumvi na mwanga unaoimarisha
na kukoleza imani ya Wakristo, vinginevyo, kashfa na mmong’onyoko wa kimaadili vinaweza
kutjitokeza na kuwa ni kikwazo kikuu kwa maisha na utume wa Kipadre.
Kuna
haja kwa Mapadre katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani kutambua, kukiri na kuimwilisha
imani yao kwa Kristo na Kanisa lake. Imani iwe ni utambulisho wa Mapadre katika maisha
yao. Imani na toba ni chanda na pete katika maisha na utume wa Mapadre anasema Kardinali
Piacenza.
Ili kutekeleza dhamana na wajibu wa kuwahudumia wengine katika imani,
kunahitaji ushuhuda wa maisha hasa kutokana na changamoto mbali mbali zinazoendelea
kujitokeza sehemu mbali mbali za dunia. Huu ni wajibu unaotekelezwa katika ngazi ya
mtu mmoja mmoja au kama Jumuiya ya waamini.
Wito na dhamana waliyokabidhwa
kutoka kwa Mwenyezi Mungu ni jambo ambalo linawataka Mapadre kufikiri na kutenda kadiri
ya wito wao. Ushuhuda wa maisha yao, uwe ni mfano bora wa kuigwa na wale wanaowazunguka
na kamwe wasiwe ni sababu ya kashfa na kuanguka kwa Wakristo. Wawe ni viongozi wenye
msimamo imara na dira makini ya kufuatwa. Daima waendelee kujifunza kutoka katika
shule ya Mama Bikira Maria, aliyefanikiwa kusikiliza kwa makini, akafanya uamuzi wa
busara na kutenda kwa hekima kadiri ya Mpango wa Mungu katika maisha yake.
Na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S., Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.