Maandiko Matakatifu yanasema kwamba, Imani inapata chimbuko lake kwa kusikiliza kwa
makini Neno la Mungu, kiasi kwamba, Biblia inapaswa kuwa ni Maktaba ya kwanza kabisa
kuwamo ndani ya Familia ya Kikristo, ili familia hizi ziweze kuonja uwepo endelevu
wa Yesu Kristo mkombozi wa dunia katika maisha na vipaumbele vyao.
Kusoma, kulitafakari
na hatimaye, kulimwilisha Neno la Mungu katika uhalisia wa maisha ya kifamilia kuna
maanisha ujenzi wa mchakato wa kurithisha imani inayofumbatwa katika ukimya wa Mwenyezi
Mungu aliyefunuliwa na Yesu Kristo. Hii ndiyo changamoto ambayo imetolewa na washiriki
wa Vyama vya Biblia kutoka sehemu mbali mbali za dunia, katika mkutano wao uliokuwa
unafanyika mjini Roma, ukiongozwa na kauli mbiu “Biblia katika familia”.
Mapokeo
ya Kanisa yanaonesha kwamba, usomaji, tafakari na umwilishaji wa Neno la Mungu katika
uhalisia wa maisha ya kifamilia ni kati ya vipaumbele vya shughuli na mikakati ya
kichungaji. Hii ni changamoto iliyotolewa na Mababa wa Kanisa kama vile Mtakatifu
Yohane Krisostom, aliyewahimiza waamini kuhakikisha kwamba, wanavalia njuga usomaji
wa Biblia katika Familia.
Askofu mkuu Vincenzo Paglia, Rais wa Baraza la Kipapa
la Familia anasema, kati ya “majanga yanayoziandama Familia nyingi za Kikristo ni
kudhani kwamba, Maandiko Matakatifu yanasomwa tu wakati wa Ibada ya Misa, Jumapili
na Siku kuu zilizoamriwa. Watu wenye hekima waliwahi kusema kwamba, dunia inasimikwa
katika nguzo kuu tatu: Biblia, Liturujia na Matendo ya huruma. Familia Takatifu ya
Yesu, Maria na Yosefu, imekuwa ni mfano bora wa kuigwa katika kutafakari Neno la Mungu,
kuimarisha imani na hatimaye, kumwilisha Neno hili katika uhalisia wa maisha.
Mtaguso
mkuu wa Pili wa Vatican, umeliwezesha Kanisa kuwarudishia tena waamini Biblia mikononi
mwao, ili Neno la Mungu liweze kuwa ni dira na mwanga katika hija ya maisha yao hapa
duniani. Hii ndiyo maana Mama Kanisa anaendelea kuwahimiza waamini kujitaabisha: kulisoma,
kulitafakari na kulimwilisha Neno la Mungu katika maisha yao, wakianzia kwenye Familia,
Jumuiya Ndogo Ndogo na kwenye Vyama vya Kitume Maparokiani.
Askofu mkuu Vincenzo
Paglia anasema, msisitizo huu umetolewa pia na Mababa wa Sinodi Maalum juu ya Neno
la Mungu iliyofanyika hivi karibuni mjini Vatican kuhusu umuhimu wa Neno la Mungu
katika maisha na utume wa Kanisa. Washiriki wa Mashirikisho ya Vyama vya Biblia, Kitaifa,
Kikanda na Kimataifa wameendelea kukazia katika mkutano wao kwamba, kuna haja kwa
Kanisa kuhakikisha kwamba, waamini wanajenga utamaduni wa kusoma, kutafakari na kulimwilisha
Neno la Mungu katika maisha na utume wao.
Wajumbe hao wanasikitika kusema kwamba,
kwa bahati mbaya, Neno la Mungu si nguzo na mwanga thabiti katika maisha ya kiroho
ya waamini walio wengi katika ulimwengu mamboleo, kinyume kabisa na Mapokeo ya Mama
Kanisa.
Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, aliwahi kuwaambia
vijana kuhakikisha kwamba, wanajenga uhusiano wa dhati kati ya Maandiko Matakatifu,
Ndoa na Familia na kwamba, maisha yao yanapaswa kuonesha Mpango wa Mungu katika Ndoa
na Familia. Waamini wajenge utamaduni wa kuwa waaminifu kwa Neno la Mungu na kati
yao wenyewe, kwani wameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu na kwamba, Mungu ana mpango
maalum katika maisha yao. Hizi ni juhudi za kuendeleza mchakato wa Uinjilishaji Mpya
katika Mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo.
Tafakari makini ya Neno
la Mungu inaweza kuwapatia mwanga wa imani na matumaini wanafamilia katika kukabiliana
na changamoto mbali mbali zinazojitokeza katika hija ya maisha yao hapa duniani. Kuna
uhusiano wa pekee kati ya Neno la Mungu, Kanisa na maisha ya Ndoa na Familia, ndiyo
maana Mama Kanisa anaendelea kuwahimiza Wanandoa kutekeleza wajibu na dhamana yao
kwa kuwalea watoto wao kadiri ya imani na mafundisho ya Kanisa, kwani wao kimsingi
ni watangazaji wa kwanza wa Neno la Mungu kwa njia ya ushuhuda wa maisha adili na
matakatifu.
Bila ya wazazi na walezi kutekeleza barabara wajibu wao ndani ya
familia, itakuwa vigumu kuweza kurithisha imani kwa vijana wa kizazi kipya. Baba Mtakatifumstaafu
Benedikto wa kumi na sita, anazialika Jumuiya za Kikristo, kuhakikisha kwamba, zinasaidia
familia kutekeleza wajibu wake wa kulea watoto katika misingi ya imani na Mafundisho
ya Kanisa.
Familia zijenge utamaduni wa kusali, kusoma na kulitafakari Neno
la Mungu katika maisha yao ya kila siku. Wazazi na walezi wawajengee watoto wao uwezo
wa kutamani na kusoma Biblia Takatifu. Biblia iheshimiwe na kutunzwa vyema. Jitihada
hizi ziendelezwe pia katika Jumuiya Ndogo ndogo za Kikristo. Wanawake wa Kikristo
wakipania kwa moyo na akili zao zote, wanaweza kuwa kweli ni vyombo makini vya kuhamasisha
usomaji na tafakari ya Neno la Mungu katika familia za Kikristo.
Familia zijitahidi
kuwa na Biblia Takatifu katika mazingira yao. Inawezekana kabisa kuwa na Biblia Takatifu
katika lugha anayoifahamu mwamini. Biblia ni Kitabu mahususi cha sala na maisha ya
Kikristo. Juhudi zinaendelea kufanyika ndani ya Kanisa ili kuhakikisha kwamba, hata
vyama vya kitume kwa watoto na vijana vinajenga utamaduni wa kusoma na kutafakari
Neno la Mungu, kwani mwelekeo huu unalenga kumjenga mtu mzima: kiroho na kimwili.
Ni
matumaini ya Askofu mkuu Vincenzo Paglia, Rais wa Baraza la Kipapa la Familia kwamba,
Familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu, itakuwa ni mfano bora wa kuigwa katika
kusoma, kulitafakari na kulimwilisha Neno la Mungu katika uhalisia wa maisha, ili
hatimaye, familia hizi ziweze kuwa kweli ni wadau wa Uinjilishaji Mpya.
Makala
haya yamehaririwa na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya
Radio Vatican.