2013-10-23 10:27:32

Nguvu ya neema: udumifu wa ndoa na majadiliano kuhusu wanandoa walioachana kuhusu kupokea Sakramenti za Kanisa


Baba Mtakatifu Francisko ametangaza Maadhimisho ya Sinodi Maalum kwa ajili ya Familia itakayofanyika mwezi Oktoba 2014, ili kuangalia kwa makini changamoto za kichungaji zinazoikabili familia katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia.

Kati ya masuala tete yanayozikabili familia nyingi ni wanandoa walioachana na kuamua kuoa au kuolewa tena. Askofu mkuu Gerhard Ludwig Muller, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Mafundisho tanzu ya Kanisa analiangalia kwa utulivu kabisa suala hili tete katika makala iliyochapishwa kwenye Gazeti la L'Osservatore Romano, linalomilikiwa na Vatican.

Kwanza kabisa analichambua tatizo hili katika misingi ya Maandiko Matakatifu, tangu Agano la Kale hadi Agano Jipya na changamoto zilizojitokeza wakati huo, hadi pale Yesu mwenyewe alipotoa msimamo thabiti kuhusu ndoa kadiri ya mpango wa Mungu katika maisha ya mwanadamu. Udumifu wa maisha ya ndoa ni agizo la Kristo mwenyewe linalofafanuliwa na Mtakatifu Paulo katika nyaraka zake mbali mbali.

Muungano kati ya mwanaume na mwanamke aliyebatizwa ni Sakramenti ya ndoa ambayo inadumu maisha yote mintarafu mpango wa Fumbo la Maisha ya Kanisa, kwani hiki ni kielelezo cha upendo mkamilifu ambao unapata chimbuko lake kutoka kwa Kristo mwenyewe. Muungano kati ya Bwana na Bibi katika kifungo cha upendo wa ndoa, kinawajalia waamini hao neema na baraka katika maisha yao.

Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki inafafanua kwamba, agano la ndoa, ambalo kwa njia yake, mwanaume na mwanamke huunda kati yao Jumuiya kwa maisha yao yote, kwa tabia yake ya asili liko kwa ajili ya mafaa yao na kwa ajili ya kuzaa na kulea watoto. Agano hili kati ya wabatizwa, limeinuliwa na Kristo Bwana kwa hadhi ya Sakramenti.

Askofu mkuu Muller anaiangalia Sakramenti ya Ndoa kadiri ya Mapokeo ya Kanisa, kwa kukazia umuhimu wa kuheshimu na kuthamini Maandiko Matakatifu na mafundisho ya Mababa wa Kanisa kuhusu udumifu wa ndoa ya Kikristo. Kwa wanandoa ambao walikuwa wameachana na wenzi wao wa ndoa walikuwa hawaruhusiwi kupokea Sakramenti za Kanisa. Suala hili lilikuwa ni tete wakati fulani katika historia ya Kanisa kiasi kwamba, kuna baadhi ya nchi ziliamua kujitenga na Khalifa wa Mtakatifu Petro kutokana na msimamo wa Kanisa Katoliki kuhusu udumifu wa Sakramenti ya Ndoa.

Umuhimu wa wanandoa kudumu katika maagano yao ni jambo ambalo pia limepewa kipaumbele cha pekee na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, Baba Mtakatifu Yohane Paulo wa Pili aliyelitaka Kanisa kutoa huduma za kiroho kwa wanandoa walioachana na kuamua kuoa au kuolewa tena Kiserikali. Lakini, Sakramenti ya Ndoa kwa upande wa Kanisa bado inaendelea kuwafunga wanandoa hao.

Ni waamini wanaopaswa kushiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa, lakini hawatarusiwa kupokea Ekaristi Takatifu, kielelezo cha upendo na uaminifu wa Kristo kwa Kanisa lake. Lengo ni kuendelea kuonesha umuhimu wa Sakramenti ya Ndoa kadiri ya Mafundisho ya Kanisa bila mkanganyiko wowote. Wanandoa walioachana na kuoana au kuolewa tena, hawawezi pia kupokea Sakramenti ya Upatanisho. Hakuna mabadiliko yanayoweza kufanywa kwa kuangalia hali za wanandoa husika.

Kumbe, wanandoa hawa wanapaswa kuongozwa na dhamiri nyofu. Sababu za kuvunjika kwa ndoa zinaangaliwa na taasisi za Kanisa zinazoshughulikia mausla ya ndoa na familia kadiri ya sheria za Kanisa. Hapa hakuna ubaguzi wa Kisakramenti bali ni uaminifu kwa Kristo na Kanisa lake. Kanisa linaendelea kuonesha masikitiko yake kutokana na mpasuko huo ambao unasababisha machungu katika maisha ya wanandoa waliotengana, lakini hata hivyo wanashauriwa kuendelea kujisikia kuwa ni sehemu ya maisha na utume wa Kanisa.

Hii ni kutokana na ukweli kwamba, upendo wa Kristo hauna ubaguzi kwa mtu awaye yote! Ni wajibu wa Jumuiya za Kikristo kuhakikisha kwamba, zinawasaidia wanandoa hawa kuanza mchakato wa toba, wongofu wa ndani na upatanisho.

Askofu mkuu Muller anasema, uamifu kati ya wanandoa ni jambo la muhimu sana katika mahusiano yao ndani ya ndoa na familia. Ni mwaliko wa kusaidiana ili kuvuka vikwazo na "majanga" yanayozinyemelea familia zao; wasimame kidete kuwalea na kuwahudumia watoto wao ambao ni zawadi kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Watoto ndio wanaoathirika kwa kiasi kikubwa pale wazazi wao wanapoamua kuvunja maagano ya ndoa yao. Wanandoa wakumbuke daima kwamba, kile ambacho Mungu ameunganisha, mwanadamu hana ruhusa ya kukitenganisha.

Hizi zote ni changamoto za maisha ya ndoa na familia, zinazopaswa kufanyiwa kazi na kupatiwa majibu muafaka kadiri ya Maandiko Matakatifu na Mapokeo ya Kanisa. Kuna sababu ambazo hata Kanisa lenyewe linazipatia uzito wa pekee hata kuruhusu ndoa iweze kuvunjwa, lakini maagano ya ndoa iliyoadhimishwa Kanisani kwa kufuata sheria na kanuni za Kanisa bado ina umuhimu wa pekee mbele ya Mwenyezi Mungu. Viongozi wa Kanisa na Jumuiya za Kikristo wawasaidie wanandoa wanaopambana na magumu katika maisha yao ili waweze kuyakabili magumu haya kwa imani, matumaini na moyo mkuu.

Askofu mkuu Muller anasema, kuna mawazo kwamba, wanandoa walioachana na kuoa au kuolewa tena waruhusiwe kupokea Sakramenti ya Ekaristi Takatifu, wakiongozwa na dhamiri nyofu, wazo ambalo lilikwishakataliwa na Kanisa. Hii inatokana na ukweli kwamba, ndoa si jambo la uhusiano wa upendo kati ya wanandoa mbele ya Mwenyezi Mungu, bali ni Sakramenti ya Kanisa na ushuhuda wa imani.

Sakramenti ya ndoa haina budi kujikita katika ukweli na kwamba, huu ni utekelezaji wa sheria ya Mungu na wala Kanisa halina mamlaka ya kwenda kinyume na sheria hii. Katika mambo yote haya huruma ya Kristo inapewa kipaumbele cha pekee kwa wanandoa wanaokabiliana na magumu katika mahusiano yao, lakini hata hapa kuna ugumu katika mafundisho ya Kanisa yanayokazia: utakatifu na haki.

Huruma ya Mungu si tiketi ya kuvunja amri za Mungu na za Kanisa. Lakini ikumbukwe kwamba, huruma ya Mungu inampatia mwamini neema ya kutubu na kuongoka baada ya kutopea katika lindi la dhambi na mauti, ili kuanza tena hija ya maisha mapya kadiri ya sura na mfano wa Mwenyezi Mungu. Mama Kanisa ataendelea kuwasindikiza wanandoa waliotengana, wakaoa au kuolewa tena katika mchakato wa uponyaji wa ndani na wokovu. Kuzuiliwa kwao kupokea Sakramenti za Kanisa ni kielelezo makini cha udumifu wa kiapo cha ndoa hadi kifo kitakapowatenganisha.

Wanandoa hawa wanapaswa kusaidiwa kwa mapana zaidi badala ya kuliangalia tatizo hili katika jicho la Sakramenti ya Ekaristi Takatifu peke yake. Kuna njia mbali mbali ambazo mwamini anaweza kuzitumia ili kujenga uhusiano wake na Mwenyezi Mungu kwa kuimarisha: imani, matumaini na mapendo. Waamini wajenge na kukoleza moyo wa toba na wongofu wa ndani; matendo ya huruma na moyo wa sala.

Mwenyezi Mungu anazo njia nyingi za kuonesha uwepo wake kwa waja wake kwani huruma na upendo wake havina mipaka. Ni jukumu kwa Jumuiya za Kikristo kuonesha moyo wa ukarimu, huruma na mapendo kwa wanandoa wanaoogelea katika shida na magumu ya maisha yao ya kiroho, ili wao pia waweze kuonja huruma na upendo wa Kristo mchungaji mwema. Kanisa linapenda kutoa huduma makini kwa wanandoa hawa, huduma ambayo inasimikwa katika ukweli na upendo.

Taarifa hii imehaririwa na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.