Serikali ya Tanzania kuboresha usafiri wa maji: Ziwa Nyasa, Tanganyika na Victoria!
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete amesema kuwa ni aibu
kwa Serikali kudaiwa na wakulima na amewahakikishia wakulima wa Wilaya ya Ludewa,
Mkoa wa Njombe, kuwa watalipwa haraka iwezekanavyo fedha zao wanazodai kwa kuiuzia
Serikali mahindi yao.
Aidha, Rais Kikwete amethibitisha kuwa meli ambazo Serikali
yake iliahidi kununua kwa ajili ya usafiri katika maziwa makuu ya Tanzania zinajengwa
na zitazinduliwa kabla ya mwaka 2015, zinaweza kuwa meli mbili badala ya moja kwa
kila moja ya maziwa ya Nyasa, Tanganyika na Victoria.
Rais Kikwete ameyasema
hayo, Jumatatu, Oktoba 21, 2013, wakati alipozungumza kwa nyakati tofauti katika ziara
yake ya Wilaya ya Ludewa, ikiwa ni mwendelezo wa ziara yake ya kikazi kukagua na kuzindua
miradi ya maendeleo katika Mkoa wa Njombe.
Rais Kikwete amewaambia wakazi wa
Ludewa kwenye mkutano wa hadhara kuwa ni kweli kuwa Serikali yake inadaiwa kiasi
cha Sh.bilioni 17 ikiwa ni deni la wakulima wa mikoa mbali mbali nchini ambao waliuza
mahindi yao ya msimu uliopita kwa kwa Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA).
Suala
hilo lilijirudia tena wakati Rais Kikwete alipokuwa anapokea Ripoti ya Maendeleo ya
Wilaya ya Ludewa ambako ameambiwa kuwa wakulima wa Wilaya hiyo pekee walikuwa bado
wanaidai Serikali Sh.bilioni 3.115 ambayo ni thamani ya mahindi tani 6,231 ambayo
wakulima hao waliiuzia NFRA.
Rais Kikwete ameambiwa kuwa mpaka sasa wakulima
wa Wilaya ya Ludewa wamelipwa kiasi cha Sh.bilioni 2.839 kutokana na tani za mahindi
tani 5,679. NFRA ilikuwa imelenga kununua kutoka kwa wakulima wa Wilaya ya Ludewa
kiasi cha tani 13,000 lakini mpaka sasa imeweza kununua tani 11,911 ingawa sehemu
kubwa ya kiasi hicho hakijalipiwa na Serikali.
“Hii ni aibu. Serikali haiwezi
kudaiwa na wakulima. Hizi fedha zitalipwa tu,” amesema Rais Kikwete na kuelezea hatua
ambazo amezichukua binafsi katika siku mbili kuhakikisha wakulima wanalipwa fedha
zao. Rais Kikwete pia amesema kuwa Serikali yake itaangalia uwezekano wa kununua
tani 2,972 za mahindi ya msimu uliopita zilizobakia mikononi mwa wakulima wa Wilaya
hiyo.
“Naambiwa kuwa bado NFRA inahitaji kiasi cha tani 40,000 hivi ili kukamilisha
shehena ya idadi ya kiasi cha tani 250,000 za mahindi kwa ajili ya Hifadhi ya Taifa
mwaka huu. Nitawaambia waangalie kama wanaweza kununua kiasi hiki kilichobakia mikononi
mwa wakulima wa Ludewa.”
Kuhusu maombi ya wananchi wa Ludewa kununua meli ya
kuchukua nafasi ya Mv. Mbeya iliyozama katika Ziwa Nyasa ili kurahisisha usafiri ndani
ya Ziwa hilo ambalo linapakana na Wilaya ya Ludewa, Rais amesema kuwa Serikali yake
inanunua meli hiyo. “Tunajua kuwa meli ya Mv. Mbeya ilizama katika Ziwa Malawi na
kwa kweli meli zimezama katika maziwa mengine makubwa ya Tanganyika na Victoria, na
mimi kwenye Kampeni niliahidi kuwa nitanunua meli moja kwa kila ziwa,” amesema Rais
Kikwete na kuongeza:
“Tumeagiza meli tatu kutoka Korea Kusini. Zinajengwa.
Tumeagiza meli nyingine tatu kutoka Denmark. Nazo zinajengwa. Hivyo, tunaweza kupata
siyo meli moja bali meli mbili katika maziwa yote matatu. Ni matumaini yangu kuwa
nitaweza kuzizindua meli hizo kabla ya kumaliza kipindi changu cha uongozi, mwaka
2015.”
Rais Kikwete pia amefafanua kuhusu kero nyingine zilizoibuliwa na wakazi
wa Wilaya ya Ludewa ikiwa ni pamoja na ujenzi wa daraja kwenye Mto Ruhuhu ambao amesema
litajengwa.