Jumuiya ya Kimataifa, sikilizeni kilio cha wananchi wa Afrika ya Kati!
Askofu mkuu Dieudonnè Nzapalainga wa Jimbo kuu la Bangui ambaye pia ni Rais wa Shirika
la Misaada la Kanisa Katoliki Jamhuri ya Watu wa Afrika ya Kati, Caritas anasema kwamba,
kwa sasa hali ya wananchi wengi nchini humo inaendelea kuwa tete kutokana na machafuko
ya kisiasa, kiasi kwamba, kuna uvunjaji mkubwa wa haki msingi za binadamu unaofanywa
na wanajeshi wa Seleka waliojitwalia madaraka mwezi Marchi, 2013.
Wanajeshi
wa Seleka wanaendelea kutuhumiwa kwa kujihusisha na vitendo vya mauaji ya kinyama,
ubakaji, ujambazi na watu wengi wamechomewa nyumba zao, shutuma ambazo zimetolewa
taarifa na wadau mbali mbali, lakini hakuna hatua za kinidhamu zilizochukuliwa na
Serikali hadi sasa.
Kutokana na hali kama hii, Askofu mkuu Nzapalainga yuko
mjini Geneva, ili kuwajulisha wanadiplomasia wanaowakilisha nchi zao kwenye Makao
Makuu ya Umoja wa Mataifa mjini Geneva na Mashirika ya Kimataifa kuhusu uvunjwaji
mkuu wa haki msingi za binadamu Jamhuri ya Watu wa Afrika ya Kati. Kanisa nchini humo
linautaka Umoja wa Mataifa kuimaarisha uwezo wa Majeshi ya kulinda amani kutoka Umoja
wa Afrika, ili wananchi waweze kuwa na uhakika wa maisha na usalama wao.
Idadi
ya Wanajeshi wa Seleka imeongezeka kutoka wanajeshi 3,500 waliokuwepo mwezi Marchi
hadi kufikia wanajeshi 25,000 kwa sasa. Kati ya wanajeshi hawa kuna idadi kubwa ya
watoto ambao wanalazimishwa kujiunga na jeshi hilo. Idadi ya silaha ndogo ndogo inazidi
kuzagaa miongoni mwa wananchi kiasi kwamba, watu wengi hawana tena uhakika wa usalama
wa maisha yao.
Zaidi ya nyumba 2,000 zimechomwa moto na familia zilizokuwa
zinaishi humo zimelazimika kutafuta makazi kwenye taasisi za kidini. Caritas inaendelea
kutoa msaada wa hali na mali, lakini kwa sasa hali hii inatisha. Viongozi wa kidini
wanaendeleza mchakato wa msamaha na upatanisho ili kujenga misingi ya haki, amani
na utulivu, mambo msingi kwa maendeleo endelevu ya watu.