2013-10-21 07:51:19

Makanisa na mchakato wa kulinda na kudumisha misingi ya haki na amani duniani


Jumuiya za Kikristo zinapaswa kujikita katika kulinda, kutetea na kudumisha misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa kweli. RealAudioMP3

Hii ni changamoto iliyotolewa hivi karibuni na Dr. Olav Fyske Tveit, Katibu mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni, wakati alipokuwa anahuhudhuria Kongamano la Kimataifa lililokuwa limeandaliwa na Baraza la Kipapa la Haki na Amani kama sehemu ya Maadhimisho ya Miaka 50 tangu Papa Yohane XXIII alipochapisha Waraka wa Kichungaji, Pacem In Terris, Amani Duniani.

Dr. Tveit anaendelea kuwaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuwa kweli ni mahujaji wa kiekumene katika mchakato wa kulinda na kudumisha haki na amani duniani, kwa kutambua kwamba, Makanisa yanashiriki kwa namna ya pekee katika mpango wa Mungu wa kulinda na kudumisha haki na amani.

Makanisa sehemu mbali mbali za dunia yanaendelea kulaani na kukemea vita na migogoro inayofuka moshi na kuendelea kusababisha maafa na majanga makubwa miongoni mwa Jumuiya ya Kimataifa. Waamini na watu wenye mapenzi mema, wanapaswa kuendelea kuzishinikiza Serikali na viongozi wao, ili kuhakikisha kwamba: haki, amani na utulivu vinapatikana kwa wote na kwamba, kama viongozi wa Jumuiya ya Kimataifa wanapaswa kusimama kidete kulinda na kutetea mafao ya wengi.

Baraza la Makanisa Ulimwenguni linajiandaa kuadhimisha Mkutano Mkuu wa Kumi, unaoongozwa na kauli mbiu “Mungu wa maisha, tuongoze katika haki na amani” Mkutano huu unatarajiwa kufunguliwa rasmi hapo tarehe 30 Oktoba hadi tarehe 8 Novemba 2013, huko Busan, Korea ya Kusini. Huu ni mwaliko kwa Jumuiya ya Kimataifa kuendeleza juhudi za upatanisho kwa Korea zote mbili, kwa kutambua kwamba, amani ni msingi mkuu wa maisha, unaoonesha upendo wa Mungu kwa binadamu wote.

Dr. Tveit anasema, amani bado iko mashakani huko Mashariki ya Kati na katika baadhi ya nchi Barani Asia kama vile Pakistan. Wakristo ambao wanaonekana kuwa ni kundi dogo katika nchi kama hizi, nao pia wanapaswa kulindwa na kuheshimiwa dhidi ya watu wenye imani na itikadi kali za kidini, wanaohatarisha usalama wa maisha ya raia wengine, kama kwamba, wao ni “wananchi wa kuja”.

Baraza la Makanisa Ulimwenguni linaendelea kutoa changamoto kwa Makanisa sehemu mbali mbali za dunia kuhakikisha kwamba, kwa pamoja wanatolea ushuhuda wa misingi ya haki, amani na upatanisho; daima wakisimama kidete kulinda, kutetea na kutunza mazingira kwani hii ni sehemu ya kazi ya uumbaji ambayo mwanadamu amekabidhiwa kuilinda na kuitunza.








All the contents on this site are copyrighted ©.