2013-10-21 07:44:57

FAO na mapambano ya janga la njaa duniani


Bwana Josè Graziano da Silva, Mkurugenzi wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa, FAO anasema, dunia ina uwezo mkubwa wa kuweza kuzalisha chakula kinachoweza kutosheleza mahitaji ya binadamu wote, lakini jambo la kusikitisha ni kuona kwamba, baa la njaa na utapiamlo limekuwa ni janga kwa mamillioni ya watu duniani, jambo ambalo kimsingi ni kashfa katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia. RealAudioMP3

Kuna haja kwa Jumuiya ya Kimataifa kujenga na kudumisha utamadhuni wa mshikamano wa dhati ili wale waliobahatika kupata neema na Baraka ya kuwa na chakula kingi waweze kugawana na “akina yakhe pangu pakavu tia mchuzi”. Inasikitisha na kuhuzunika kusikia na kushuhudia watu wakitafuta makombo ya chakula kilichotupwa jalalani! Ni changamoto hizi ambazo Baba Mtakatifu Francisko alizotoa alipokutana na wajumbe wa FAO walipomtembelea mjini Vatican hapo tarehe 30 Juni 2013.

Historia inaonesha kwamba, ushirikiano wa dhati kati ya wakulima, wafugaji, wanasayansi na wahandisi, wamefanikiwa kuhakikisha kwamba, kunakuwepo na uzalishaji wa chakula cha kutosha kutokana na ongezeko la idadi ya watu wa duniani. Tangu baada ya Vita Kuu ya Pili ya Dunia, idadi ya atu imeongezeka maradufu, lakini uzalishaji wa chakula umeongezeka kwa asilimia 40% . Haya ni mafanikio makubwa katika mapambazo ya Karne ya 21. Lakini ongezeko hili la uzalishaji wa chakula linakwenda sanjari na utupaji mkubwa wa chakula ambacho kingetumika kwa ajili ya kuganga njaa kwa watu wanaoendelea kutumbukia katika janga la njaa duniani.

Maendeleo ya sayansi na teknolojia yamechangia kwa namna ya pekee kuchakaa kwa ardhi kutokana na uwepo wa matumizi mabaya ya ardhi, maji na misitu. Mambo haya yamepelekea pia kupungua kwa uwepo wa uhakika wa usalama wa chakula duniani. Kuna makundi makubwa ya watu yanalazimika kuyakimbia makazi nan chi zao kutokana na baa la njaa na watoto wengi wanaendelea kupoteza maisha kutokana na utapia mlo wa kutisha. Kutokana na kilio kama hiki, kuna haja kwa Jumuiya ya Kimataifa kuhakikisha kwamba, inaibua mbinu mkakati utakaoweza kuhakikisha uwepo wa usalama wa chakula kwa sasa na kwa vizazi vijavyo, sanjari na kuhakikisha kwamba, watu million 870 wanaokabiliwa na baa la njaa kwa sasa wanapata chakula.

Bwana Graziano da Silva anabainisha kwamba, idadi kubwa ya watu wanaokabiliwa na baa la njaa wanaishi katika nchi zinazoendelea duniani. Janga la njaa linaanza kupiga hodi kwa kasi hata katika nchi tajiri kutokana na athari za myumbo wa uchumi kimataifa. Baa la njaa linapukutisha maisha na matumaini ya maisha kwa mamillioni ya watu duniani. Dhana ya uhakika wa usalama wa chakula inapania kuhakikisha kwamba, kila mtu anakuwa na uhakika wa chakula ili aweze kupata maisha bora na endelevu.

Anasema, katika makala aliyoiandika kwenye Gazeti la L’Osservatore Romano, linalotolewa na Vatican kila siku kwamba, Kanisa limewekeza kwa kiasi kikubwa katika masuala ya afya ya mwanadamu, kama ilivyo pia kwa dini mbali mbali duniani. Lakini, bado kuna watu ambao wanashinda na kulala njaa kwa kukosa chakula, changamoto kwa waamini wa dini na madhehebu mbali mbali duniani kujenga na kuimarisha utamaduni wa upendo na mshikamano kwa jirani zao, walioumbwa kwa sura na mfano wa Mungu; watu wanaopaswa kuonjeshwa upendo kadiri ya Maandiko na Misaafu mitakatifu.

Inasikitisha kuona kwamba, ubinafsi, uchoyo na tamaa ya fedha vinaendelea kuwa ni kizingiti katika mchakato wa kuwa na uhakika wa usalama wa chakula duniani, kiasi cha dunia kuendelea kushuhudia mamillioni ya watu wakiteseka na kufariki dunia kutokana na baa la njaa na utapia mlo wa kutisha. Kuna baadhi ya watu wanadhani kwamba, njaa haiwezi kupatiwa ufumbuzi na kwamba, hii eti ni sehemu ya maisha ya binadamu, jambo ambalo linapingwa vikali na Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Chakula Duniani kwa Mwaka 2013.

Baa la njaa na utapiamlo ni matokeo ya umaskini wa hali na kipato unaokwamisha jitihada za familia nyingi kujijengea uwezo wa kununua au kuzalisha chakula bora na cha kutosha kwa ajili ya matumizi ya familia zao. Baa la njaa linakwamisha mchakato wa maendeleo endelevu kwani hakuna hata siku moja mtu mwenye njaa atakayeweza kuzalisha kwa wingi au kusoma, akaelewa na kuhamasika zaidi. Kumbe, kuna haja ya kuhakikisha kwamba, watu wanapata fursa ya kupata chakula kwani chakula cha kutosha kipo!

Watu watambue kwamba, chakula ni haki ya kila mtu! Mapambano dhidi ya baa la njaa ni jambo linalowashirikisha wadau mbali mbali na wala si kwa ajili ya Serikali pekee! Kila mtu atekeleze wajibu na dhamana yake, hapo baa la njaa litaweza kufutika kama ndoto ya mchana! Jamii ijenge ushirikiano wenye tija na utengamano; mshikamano unaojali na kuwajibisha kwa kuwashirikisha wakulima wadogo wadogo na wanawake kuchangia katika mchakato wa kuwa na uhakika wa usalama wa chakula kimataifa. Brazil imeweza kufuta baa la njaa, jambo hili pia linawezekana kwa nchi nyingine duniani!

Wakulima wadodo wakiwezeshwa pamoja na mpango wa chakula kwa wanafunzi wa shule za msingi ni mikakati inayoweza kuboresha maisha ya wananchi wengi duniani sanjari na kupunguza vifo vya watoto wachanga kutokana na utapiamlo wa kutisha. Watoto wa shule watahamasika kusoma zaidi na nguvu kazi itaendelea kufaidi matunda ya jasho lake, kumbe, kilio cha maboresho ya uhakika wa usalama wa chakula duniani anasema, Bwana Josè da Silva una faida kubwa kwa Jamii husika na maendeleo ya wengi.

Jumuiya ya Kimataifa inapaswa kujenga utamaduni wa kuhifadhi chakula kwani chakula kingi kinachozalishwa kinapotea tangu wakati mazao yakiwa shambani hadi pale yanapowafikia walaji. Watu wanamwaga chakula kingi, chakula ambacho kingeweza kutumika kwa ajili ya maskini. Jamii ijifunze kujenga utamaduni wa kulinda na kutunza mazingira ili kudhibiti athari za mabadiliko ya tabia nchi. Wazazi pia wawajengee watoto wao tabia ya kula vyema na chakula bora. Wasiridhike kuwaona watoto wamenenepa na kuwa na vitambi, wakadhani kwamba, huo ndiyo ustaharabu wa ulimwengu mamboleo!

Bwana Graziano da Silva Mkurugenzi mkuu wa FAO anasema, Serikali kwa sasa zihakikishe kwamba, wananchi wao wanakuwa na uhakika wa usalama wa chakula ili waweze kuchangia katika ustawi na maendeleo yao. Kila mdau akitekeleza wajibu wake, baa la njaa linaweza kupewa kisogo duniani!

Imehaririwa na
Padre Richard A. Mjigwa,
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.