China kuwekeza zaidi katika sekta ya utalii nchini Tanzania
China imeahidi kuleta nchini Tanzania watalii 30,000 katika kipindi cha miaka mitatu
kuanzia mwakani. Ahadi hiyo imetolewa Jumapili, Oktoba 20, 2013 na Mwenyekiti wa Wakala
wa kutoa huduma za usafiri wa China na Hong Kong (China Travel Services - Hong Kong
Limited - CTS) Bw. Zhang Xuewu alipofanya mazungumzo na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda
jijini Shenzen, China.
Alisema kampuni yake itawandaa mawakala wa usafirishaji
watalii ili kuhakikisha kuwa watalii 10,000 wanapatikana kila mwaka ambao kiu yao
ni kuja Tanzania. “Wengi wanapenda kutembelea mbuga, lakini hapa nchini wamezoea kuona
walio sakafuni, wakija watawaona wanyama live” (akimaanisha kuwa Wachina wamezoea
kuona wanyama wa sanamu kwenye makumbusho yao hapa jiji la Shenzen).
Waziri
Mkuu ambaye yuko katika siku ya tano ya ziara yake ya kikazi ya siku tisa kwa mwaliko
wa Serikali ya China alisema haelewi ni kwa nini kampuni hiyo imeweza kupeleka watalii
Afrika Kusini na nchi jirani za Afrika Mashariki wakati haina urafiki nazo lakini
imeshindwa kuwaleta Tanzania kwenye ambayo ina mahusiano mazuri na ya muda mrefu.
Akizungumza
na Bw. Xuewu pamoja na baadhi ya viongozi kutoka Tanzania alioambatana nao, Waziri
Mkuu alisema amepewa maelekezo rasmi na Rais Jakaya Kikwete ya kufuatilia suala la
watalii wa kutoka China hasa ikizingatiwa kwamba mazungumzo ya jambo hili yalianza
wakati wa Rais wa awamu ya tatu, Ndugu Benjamin Mkapa.
“Katika bara la Afrika
hakuna nchi yenye vivutio lukuki kama Tanzania. Na tovuti ya www.safaribooking.com
imeitangaza Tanzania kuwa nchi inayofaa kwa safari za mbugani kama mtu anataka kuona
vivutio vizuri na vya asili. Sasa ni kwa nini hatupati watalii wa kutosha na tunafanyaje
ili kubadilisha hali hiyo?,” alihoji.
Alisema njia mojawapo ni kuhakikisha
kuwa kunakuwa na ndege ya moja moja kutoka miji ya China hadi Dar es Salaam jambo
alisema litasadia kupuinguza kero kwa wasafiri ambao hivi sasa inabidi waunge safari
mara mbili hadi tatu ili kufika Tanzania. “Tuangalie uwezekano wa kuwa na ndege ya
moja kwa moja kutoka China hadi Dar es Salaam au Arusha... wenzetu Kenya na Afrika
Kusini wameweza kupata watalii wengi sababu wana ndege za moja kwa moja,” alisema.
Alimshawishi
Mwenyekiti huyo aangalie pia uwezekano wa kujenga mahoteli katika mikoa ya Tanzania
ili kupunguza uhaba wa vyumba punde watalii wakianza kufurika. Pia alimhakikishia
fursa ya kujenga uwanja wa gofu chini ya mlima Kilimanjaro kwani yote mawili ni maeneo
ambayo kampuni yake inao uwezo wa kufanya kama sehemu ya majukumu yake.
Pia
alimpa wazo kwamba kama sehemu ya maadhimisho ya miaka 50 ya urafiki baina ya Tanzania
na China, CTS inaweza kuandaa kundi kubwa la wakala wakaja Arusha na kufanya mkutano
wa siku mbili au tatu na kisha wakapata fursa ya kujadili namna ambavyo Tanzania na
China zinaweza kushirikiana kukuza suala la utalii. “Mkimaliza mkutano wenu mnasaini
makubaliano baina yenu na Bodi ya Utalii, mambo yanasonga mbele,” aliongeza.
Kwa
upande wake, Bw. Xuewu alikiri kuwepo kwa mazungumzo ya wakuu wa nchi akisema: “Mwaka
2004, Rais Hu Jintao alifikia makubaliano na Rais (Benjamin) Mkapa kwamba watafungua
milango ya utalii kwa Tanzania. Mwezi Machi, 2013, Rais Kikwete na Rais wa China,
Bw. Xi Jinping walirudia tena mazungumzo hayo na kukubaliana kuwa Tanzania itapewa
kipaumbele cha pekee kwa watalii wa kutoka China.
“Na hata wewe na Waziri Mkuu
wetu, Bw. Li Keqiang, mwezi huu mmeshuhudia mawaziri wakisaini makubaliano kuhusiana
na suala hilo, kwa kweli kama Serikali mmedhamiria kuhakikishia kuwa mnainua viwango
vya utalii ili kukuza uchumi na kuleta maendeleo kwa Watanzania,” alisema.
Alimshukuru
Waziri Mkuu kwa wazo lake kuhusu mkutano na MoU na kumhakikishia kuwa wako tayari
kujenga hoteli, viwanja vya gofu, kuanzisha tawi la kampuni yao ya uwakala kama ambavyo
Waziri Mkuu amewasahauri.