2013-10-18 12:15:08

Utetezi wa haki msingi za binadamu ni msingi thabiti wa mapambano dhidi ya umaskini duniani!


Jumuiya ya Kimataifa hapo tarehe 17 Oktoba 2013 imeadhimisha Siku ya Kupambana na baa la umaskini duniani, iliyoongozwa na kauli mbiu "kufanya kazi kwa pamoja ili kuondoa ubaguzi: kwa kujenga kutokana na uzoefu na ufahamu wa watu wanaoishi katika umaskini wa kutupwa".

Jumuiya ya Kimataifa imetafakari, lengo la kwanza la Maendeleo ya Millenia, ifikapo mwaka 2015, ili kuondokana na baa la njaa sanjari na maboresho ya huduma ya afya. Takwimu za Shirika la kuhudumia watoto la Umoja wa Mataifa, UNICEF zinaonesha kwamba, bado kuna idadi kubwa ya watoto wenye umri chini ya miaka mitano wanaofariki dunia kila siku kutokana na utapiamlo wa kutisha.

Maadhimisho ya Siku ya Chakula Duniani na Siku ya Kupambana na Baa la Umaskini Duniani ni changamoto kwa Jumuiya ya Kimataifa kuhakikisha kwamba, mambo haya mawili yanapatiwa ufumbuzi wa kudumu, kama sehemu ya mchakato wa kulinda na kudumisha haki msingi za binadamu. Baa la umaskini duniani linawanyima watu wengi fursa ya kupata rasilimali, kutumia kikamilifu uwezo wao katika kupambana na hali ya maisha; ukosefu wa usalama na mahitaji msingi. Matokeo yake ni kushindwa kuchangia kwa kiasi kikubwa katika medani mbali mbali za maisha.

Jumuiya ya Kimataifa inaalikwa kwa namna ya pekee, kutoa kipaumbele cha kwanza kwa utu na heshima ya binadamu sanjari na kuondokana na falsafa ya ubaguzi ambayo imekuwa ni chanzo kikubwa cha majanga katika maisha ya Jamii nyingi duniani. Utetezi wa haki msingi za binadamu ni msingi thabiti wa mapambano dhidi ya baa la umaskini pamoja na kuziwezesha familia kutekeleza dhamana na wajibu wake ndani ya Jamii.







All the contents on this site are copyrighted ©.